TUME YA HAKI ZA BINADAMU YATAKA WAALIMU KENYA KUSITISHA MGOMO WAO

Nyamira
Walimu katika kaunti ya Nyamira wakiandamana barabara ya Nyamira- Kisii. Picha/HENRY NYARORA 

Na CHARLES WASONGA

TUME ya kitaifa ya kutetea haki za kibinadamu (KNCHR) inawataka walimu warejee kazini, ikisema mgomo wao unawanyima watoto haki ya kupata elimu kama ilivyoangaziwa katika kifungu 53 cha Katiba.
Kaimu mwenyekiti wa Tume ya Kitaifa ya Haki za Kibinadamu (KNHRC) Bi Anne Kyalo  hata hivyo alisema tume hiyo inaunga mkono matakwa ya walimu hao ya kutaka walipwe  nyongeza ya marupurupu  kulingana na mkataba kati yao na Serikali mnamo 1997.

“Japo tunaunga mkono matakwa ya walimu, tunaunga mkono matakwa yao kwani mkataba wao uliafikiwa kwa mujibu wa sheria. Lakini tunawaomba kurejea kazini huku viongozi wao walijadiliana na Serikali kuhusu njia za kutanzua mzozo huo ili watoto wasiendelee kuathirika kimasomo,” akasema Bi Kyalo.

Hata hivyo, tume hiyo iliiakshifu Serikali kwa kutisha kutowalipa takriban walimu 240,000 wanaogoma mishahara yao ya mwezi Juni, ikisema hiyo ni dhuluma na ukiukaji wa haki za walimu hao. “Tunapinga vitisho kama hivi dhidi ya walimu kwani hii ni kinyume na haki zao kama ilivyofafanuliwa katika kipengee cha 41 ibara ya 2 (c) na (d) cha Katiba,” akaongeza kamishna huyo.

Wakati huo huo, tume hiyo alipinga mradi wa Serikali wa kutoa tarakilishi ndogo (Laptops) kwa wanafunzi wa darasa la kwanza kuanzia hapo mwakani ikisema kuwa, Serikali ingeshughulikia changamoto zinazokabili shule za msingi kwanza.

“Ingawa wazo hilo ni bora, hasa ikizingatiwa kuwa hii ni enzi ya teknolojia ya mawasiliano, shule nyingi nchini hazina walimu wa kutosha vifaa vya masomo na hata madarasa. Haya ndio mahitaji ambayo Serikali ingepania kushughulikia wala sio tarakilishi ambayo itaigharimu Serikali pesa nyingi, “ akasema Afisa Mkuu Mtendaji wa tume hiyo Bi Patricia Nyaundi.

Alipendekeza kuwa masomo ya kompyuta yafunzwe wanafunzi kuanzia kiwango cha darasa la nne na wala sio darasa la kwanza kutokana na changamoto za kutoa mafunzo hayo. “Nakumbuka katika miaka ya zamani, ni wanafunzi wa darasa la nne kwenda juu ndio walikuwa wakiagizwa kutumia kalamu ya wino.

Wale wa darasa la kwanza hadi tatu walikuwa wakitumia penseli, “ akasema huku akipendekeza mfumo kama huo utumiwe kuanzisha masomo ya tarakilishi katika shule za msingi za umma.

Tume hiyo ilibashiri kuwa huenda uagizaji wa tarakilishi hizo ukakumbwa na kashfa kama ilivyoshuhudiwa mwaka jana wakati wa uagizaji wa vifaa vya kusajili wapiga kura kielektroniki (BVR) ambayo sasa inachunguzwa na Tume ya Maadili na Vita dhidi ya Ufisadi (EACC)


JIUNGE NA EDMO BLOG SASA

Usipitwe!! Jiunge nasi kupitia Facebook,Twitter na Instagram ili kupata habari zote za town! Usikose kujiunga na Youtube kuangalia video zote kali kutoka Edmo Blog Pekee!, kujiunga bonyeza hapa>>>Youtube

Tupe Maoni Yako lakini Usiandike Matusi



 
© Copyright EDMO BLOG | Designed By Peruzibongo