
Kisa hicho
cha kushangaza kilitokea katika kanisa la Taru, Dayosisi Kuu ya Mombasa
na kupelekea Padri Thomas Apil kukabiliwa vikali na waumini
Ilibidi polisi kutoka kituo cha Taru kuitwa kumuokoa padri huyo asiumizwe na waumini wake.
Padri Api
amekuwa na mgogoro katika parishi ya Taru tangu ahamishiwe huko mwaka
mmoja uliopita kuchukua mahali pa Padri Henry Katana ambaye alipata
uhamisho wa ghafla.
Afisa Mkuu wa
polisi wilayani Kinango Bw Silas Ringera alisema ilibidi awatume
maafisa wake kumuokoa padre huyo kutokana na fujo baada ya kuleta jeneza
kanisani na kuzuia waumini kuingia kwa misa.
Jumapili
iliyotangulia, waumini waliokuwa na hasira walifunga nyumba ya padri
huyo na kanisa na kumuamuru aondoke. Hata hivyo, walishangaa walipomuona
amebeba jeneza hapo Jumamosi jioni ambalo alilitumia kuzuia waumini
kuingia kanisani
“Padre huyo
aliandamana na wanafunzi wawili wa seminari ambao aliingia nao kanisani
na kuendesha ibada baada ya kufunga kanisa kwa jeneza,” alisema mwumini.
Padri Apil alivaa nguo nyekundu siku hiyo.
Akiongea
baada ya kisa hicho, padri huyo alisema alipotumwa kuhudumu mahala hapo
hakupokelewa vyema. “Najua ni kwa sababu mimi sitoki katika jamii ya
Wamijikenda kama alivyokuwa Padri Henry Katana,” alisema.
Lakini waumini walipuuzilia mbali madai hayo wakisema padri huyo ndiye aliyejiletea shida.
Walisema mapadri wengi wakiwemo Wazungu na kutoka makabila mbalimbali washahudumu hapo pasipo matatizo.
Walimlaumu
padri huyo kwa tabia isiyoridhisha kama vile kuleta wanawake nyumbani
kwake na kuvunjilia mbali mashirika yote ya kanisa hilo.
Mwenyekiti wa
kamati ya parokia hiyo Bw Raphael Galuka majuzi aliongoza ujumbe
kumuona Askofu Lele na kumtaka amhamishe padri huyo. Hata hivyo, askofu
huyo hakuchukua hatua yoyote.