ULEVI WAWATHIRI WATANZANIA KWA ASILIMIA 31


ASILIMIA 26.8 hadi asilimia 31.9 ya Watanzania wanatumia pombe na asilimia 27.4 kati ya hao ambao ni wanaume na wengine asilimia 13.4 ambao ni wanawake, ni walevi wa kupindukia. Bunge lilielezwa jana.

Takwimu hizo zilitolewa na Naibu Waziri wa Afya na Ustawi wa Jamii, Dk Seif Rashid, ambaye alisema kuwa viwango hivyo vimetokana na utafiti uliofanywa kati ya Februari hadi Oktoba mwaka jana 2012.

Kwa mujibu wa naibu waziri, utafiti huo ulifanywa na Shirika la Afya Duniani (WHO).

Alikuwa akijibu swali la Abdallah Haji Ali (Kiwani–CUF) aliyetaka kujua kauli ya Serikali kuhusu utumiaji wa pombe ambao umethibitika kuwa ni hatari kwa afya za binadamu. Pia alipendekeza pombe ipigwe marufuku kabisa hapa nchini kwa kuzingatia madhara yake.

Naibu waziri alisema tafiti zimeonyesha kuwa watu milioni mbili wanafariki dunia kila mwaka duniani kutokana na madhara ya matumizi ya pombe na asilimia nne ya matatizo ya kiafya yanatokana na matumizi ya pombe.

“Hali inazidi kuwa mbaya zaidi katika nchi zinazoendelea hasa kutokana na kukabiliwa na hali mbaya ya kiuchumi na ustawi wa jamii inayochangiwa na magonjwa ya malaria, kifua kikuu na Ukimwi,” alisema Dk Rashid.
CHANZO:MWANANCHI


JIUNGE NA EDMO BLOG SASA

Usipitwe!! Jiunge nasi kupitia Facebook,Twitter na Instagram ili kupata habari zote za town! Usikose kujiunga na Youtube kuangalia video zote kali kutoka Edmo Blog Pekee!, kujiunga bonyeza hapa>>>Youtube

Tupe Maoni Yako lakini Usiandike Matusi



 
© Copyright EDMO BLOG | Designed By Peruzibongo