Mwenyekiti wa CWT Makete Mwl. Lutangilo Sanga (kulia) akizungumza na mwandishi wa habari hii
Ikiwa zimepita siku kadhaa sasa tangu kufanyika sikukuu ya wafanyakazi, kumeibuka sintofahamu katika chama cha waalimu(CWT) wilaya ya Makete kutokana na kuwepo tuhuma kuwa baadhi ya waalimu waliuziwa fulana zilizotolewa na chama hicho taifa kwa ajili ya kusherehekea kinyume na makubaliano
Hii inatokana kuwepo baadhi ya waalimu kudai kuwa waliuziwa
fulana hizo kwa shilingi 1,000/= kwa fulana moja tofauti na agizo la CWT makao
makuu kuwa waalimu wote wapewe fulana za Mei mosi bure
Kutokana na minung’uniko iliyokuwa ikitolewa na watu
wanaosadikika kuwa ni waalimu ambao hawakutaka kutaja majina yao, ripota wetu
alilazimika kumfuata mwenyekiti wa chama cha waalimu wilaya ya Makete Bw.
Lutangilo Sanga ambaye bila kumumunya maneno alimtwisha lawama katibu wa chama
hicho wilaya ya Makete kuwa ndiye aliyepokea shilingi elfu moja moja za fulana
hizo
Mwenyekiti huyo alisema amesikia tetesi hizo ambapo pia
alipigiwa simu na baadhi ya waalimu ambao hakuwataja, ambao walimpa malalamiko
yao kuwa wameuziwa fulana za Mei mosi licha ya kuwa na taarifa kuwa fulana hizo
walitakiwa kupewa bure, jambo alilosema hakuwa na majibu nalo kwa kuwa katibu
wake ndiye alikuwa akilishughulikia
Mwenyekiti huyo alikwenda mbali zaidi na kudai kuwa katibu
wake amekuwa akifanya baadhi ya mambo bila kumshirikisha na ndiyo maana yeye
anakosa majibu, lakini alipoulizwa na mwandishi wetu kuwa kama mwnyekiti
amechukua hatua gani kama katibu wake hamshirikishi, hakuwa na jibu
“Mimi nifanyeje kama hanishirikishi na ndiyo maana yanatokea
kama haya” alisema
Mtandao huu ulilazimika kumfuata Katibu wa chama cha waalimu
wilaya ya Makete aliyejitaja kwa jina moja la Kapinga na kushangazwa na taarifa
hizo huku akisema kuwa hajauza hata fulana moja kwa waalimu na kama wapo
waalimu waliouziwa fulana wakadai fedha zao
| Katibu CWT Makete |
“Ndugu mwandishi wa habari orodha ya waliopokea fulana za
mei mosi hizi hapa, na hawa ndio wamepokea kutoka kwangu, mimi wakati nagawa
fulana nilikuwa naonana na viongozi tu, kama ni mratibu elimu, ama mwakilishi
yeyote namkabidhi fulana na kofia za kata ama shule yake, anasaini naondoka,
kama orodha hii( huku akiionesha) ilivyo sasa huo uuzaji unatoka wapi” alisema
Kapinga
Alisema kama kuna mwalimu yeyote ambaye ameuziwa fulana na
katibu huyo ajitokeze hadharani, na yuko tayari kuwajibika kwa hilo kama ni
kweli yeye amewuzia waalimu fulana, huku akisema yeye kama mtendaji mkuu wa
chama hajapokea malalamiko yoyote ofisini kuhusu waalimu kuuziwa fulana
Ameongeza kwa kuwa yeye alikuwa akigawa fulana hizo kiujumla
kulingana na idadi ya waalimu wa shule, inawezekana wapo baadhi ya waliozipokea
halafu wakaenda kuziuza kwa waalimu, ambapo kosa si lake bali ni la aliyeuza
ingawa anafahamu kuwa zinapaswa kutolewa bure, na aliyefanya hivyo anapaswa
kurejesha fedha za mwalimu huyo na hatua nyingine zitafuata
Kuhusu tuhuma kuwa amekuwa akijiamulia mambo bila
kumshirikisha mwenyekiti wake, katibu huyo alisema si kweli na badala yake
asema yeye mwenyekiti ndiye amekuwa akijiamulia mambo mwenyewe ikiwemo kuitisha
vikao ilihali muitishaji wa vikao ni katibu kama katiba ya chama inavyoelekeza
“Mfano mzuri ni hii barua hapa ameitisha kikao na amesaini,
bila hata kunishirikisha ilihali mimi katibu ndiye muandaaji wa vikao kwa
kushirikiana na yeye, sasa yeye kawaita wajumbe kwa barua hii na kufanya kikao,
sasa hapo nani hamshirikishi mwenzie” alisema Kapinga
