WILAYA YA SIMANJIRO YAJIPANGA KURUDI KWENYE HADHI YAKE KIELIMU

 
Imebainishwa kuwa kwa muda wa miaka minne mfululizo  wilaya ya Simanjiro mkoani Manyara ilikuwa inashika nafasi ya kwanza kwa kiwango cha ufaulu mkoani humo imejipanga kurudia nafasi hiyo baada ya mwaka jana kushika nafasi ya tano.
 
Hayo yamebainishwa na  mwenyekiti wa halmashauri ya wilaya hiyo Peter Tendee wakati akifunga kikao cha kawaida cha baraza la madiwani hao kilichofanyika mji mdogo wa Orkesumet wilaya simanjiro mkoani Manyara.
 
Alibainisha kuwa  tangu mwaka 2008 wilaya hiyo ilikuwa inakamata nafasi ya kwanza mkoani humo kwa kufaulisha vizuri wanafunzi wanaomaliza darasa la saba na kuingia kidato cha kwanza lakini mwaka jana walishika nafasi ya tano.
 
Aliongeza kuwa  jitihada na juhudi za makusudi zinahitajika kufanyika kwa ushirikiano wa viongozi,walimu,wazazi,walezi na wanafunzi wenyewe ili waweze kurudia tena kwenye nafasi yao ya kwanza kama miaka iliyopita.
 
Alisema kuwa zipo changamoto mbalimbali zinazowakabili kwenye wilaya hiyo ikiwemo wanafunzi kupata ujauzito,utoro na umbali wa shule na makazi hivyo wanapaswa wapambane ili kuweza kuzimaliza changamoto hizo.
 
Kwa upande wake mmoja wa mjumbe wa Kamati ya Elimu Afya na Maji Clempu Ole Kinoka alisisitiza kuwa  kaimu Mkurugenzi wa halmashauri Patrice Saduka aandike barua kwa kamati ya mitihani ya mkoa juu ya wanafunzi waliodaiwa kufaulu na hawajui kusoma na kuandika,wana uwezo huo baada ya kufanya mtihani. 
 
 Aliendela kusema kuwa  orodha ya wanafunzi wa darasa la saba ambao hawakufanya mtihani wa Taifa mwaka jana,ichambuliwe na maofisa watendaji wa vijiji,kata na waratibu ili wazazi wanaostahili kupelekwa Mahakamani wajulikane.
 
 Alisema kuwa orodha ya wazazi wanaotakiwa kupelekwa Mahakamani kutokana na watoto wao kutofanya mtihani wa darasa la saba mwaka 2012 ipelekwe kwenye Kamati ya Fedha Uongozi na mipango mwezi huu wa Februari.
 
 Aidha matokeo ya darasa la saba ya mwaka 2012  yalisababisha madiwani kumkataa aliyekuwa Ofisa elimu wa wilaya hiyo,Jackson Mbise aliyewashusha vyeo walimu wakuu 15 wa shule zilizofaulisha wanafunzi wasiojua kusoma na kuandika. 
 
 Pia  mwaka 2012/2013 halmashauri ya mji wa Babati ilishika nafasi ya kwanza mkoani humo kwa kiwango cha ufaulu na kufuatiwa na halmashauri za wilaya ya Mbulu,Babati vijijini,Hanang’,Simanjiro na Kiteto.


JIUNGE NA EDMO BLOG SASA

Usipitwe!! Jiunge nasi kupitia Facebook,Twitter na Instagram ili kupata habari zote za town! Usikose kujiunga na Youtube kuangalia video zote kali kutoka Edmo Blog Pekee!, kujiunga bonyeza hapa>>>Youtube

Tupe Maoni Yako lakini Usiandike Matusi



 
© Copyright EDMO BLOG | Designed By Peruzibongo