
Utangulizi
Kumekuwepo
na taarifa kupitia baadhi ya vyombo vya habari kwamba kuna upungufu
mkubwa wa dawa mseto za kutibu malaria aina ya ALU katika vituo vya
kutolea huduma za afya hapa nchini.Taarifa hizo zilimnukuu Mkurugenzi wa
shirika lisilo la serikali la SIKIKA, katika mkutano na wahariri wa
vyombo vya habari uliofanyika mjini Dar es Salaam hivi karibuni.
Ufafanuzi
Taarifa
alizotoa Mkurugenzi wa SIKIKA, chanzo chake kimetokana na kunukuu
taarifa zinazopatikana kutoka katika mfumo wa kielektroniki wa wizara
ambao unafuatilia takwimu za dawa za malaria katika vituo vya huduma
ujulikanao kama ‘SMS for Life’.
Mfumo
huu unatoa taarifa za upatikanaji wa dawa za kutibu malaria aina mbili
tu ambazo ni Alu na Quinine, na sio dawa nyingine za kutibu Malaria.
Hivyo
basi, dawa zingine zote pamoja na zile za msaada, ambazo zinapokelewa
na kusambazwa katika hospitali zote nchini hazitolewi taarifa kwa
kutumia mfumo huu wa “SMS for Life”. Hivyo kusababisha wakati mwingine
kuonekana hakuna dawa wakati dawa hizo zipo vituoni.
Hali halisi
Dawa za Alu zilizopokelewa mwezi Januari 2013;-
- Vidonge vya watoto dozi 2,400,000 ambazo zitatosheleza kwa miezi 5
- Vidonge vya watu wazima dozi 5,688,720 zinatosheleza matumizi ya miezi 14
Shehena nyingine za dawa za Alu zinatarajiwa kufika nchini mwezi Machi, 2013.
Aidha,
kufikia tarehe 31 Disemba 2012 kulikuwa na dawa za Alu za watoto dozi
1,315,967 ambazo zilitosha matumizi ya miezi 2. Vile vile, kulikuwa na
dozi za Alu 2,283,610 za watu wazima ambazo zinatosha matumizi ya miezi 2
na nusu.
Hitimisho
Wizara
inapenda kuwahakikishia wananchi kwamba kwa sasa kuna dawa za kutibu
malaria vituoni za kutosha. Vile vile, Bohari kuu ya Dawa (MSD)
inaendelea na usambazaji wa dawa hizi katika vituo vyote nchini. Aidha,
taratibu za kuagiza na kuleta shehena zaidi ya dawa za malaria kutoka
nje ya nchi zinaendelea ili kuhakikisha kuwa dawa za kutibu malaria
zinapatikana kwa muda wote.
Regina L. Kikuli
KAIMU KATIBU MKUU
01/02/2013