WANAFUNZI WA IFM WAELEZEA KIBANO WALICHOKIPATA KIGAMBONI

 
Askari wa kike na wakiume wakimdhibiti kwa bakora na marungu mwanafunzi wa chuo cha IFM (mwenye nguo za blue) baada ya kumchomoa kwenye jengo alilojificha ili kukwepa mabomu ya machozi.
 
Huyu alishikiliwa mapema mara baada ya mabomu kuanza kupigwa, huku akionja joto ya jiwe ya askari hao ambao walionekana kuwa na uchu wakupiga.
 
SIKU moja baada ya wanafunzi wa Chuo cha Usimamizi wa Fedha (IFM), kuitisha maandamano kushinikiza ulinzi wa polisi kutokana na vitendo vya udhalilishaji, jana walielezea jinsi wanavyofanyiwa vitendo hivyo na wahuni.

Wanafunzi hao ambao wamepanga katika nyumba zilizoko Kigamboni, wamedai kudhalilishwa na wahuni hao kwa kuporwa vifaa vyao kama kompyuta, fedha na vitu vingine na hata kubakwa na kulawitiwa.

Rais wa Serikali ya Wanafunzi IFM (IFMSO), Michael Charles jana alieleza jinsi udhalilishaji dhidi ya wanachuo wawili wanaume wa chuoni hapo ulivyotokea Januari 12, mwaka huu.
“Kulikuwa na wanafunzi wanne walikuwa wakijisomea chumbani kabla ya kuvamiwa usiku wa manane na watu wasiowatambua wapatao wanane.”

“Watu hao walikuwa wanataka kompyuta, simu, fedha na vitu vingine na vile ambavyo hawakuwa navyo, walizua tafrani kati yao... Hawa jamaa walikuwa kwenye nyumba yao iliyoko Uwanja wa Machava.”


“Katika sakata hilo, wanafunzi wawili walipata upenyo na kukimbia, lakini wawili walikosa na kuendelea kupambana na wahuni hao ambao waliwazidi nguvu kutokana na wingi wao na kuwaingilia kinyume na maumbile.”

“Kwa kweli ilituuma sana baada ya kupata bahari zile. Waliwadhalilisha sana... Jamaa walipora mali za wanafunzi hao na zaidi ni kompyuta, fedha na simu. Tumekuwa tukiripoti matukio haya mara kwa mara polisi, lakini hakuna hatua zozote zilizochukuliwa kwani vitendo hivi ni vya muda mrefu.”

“Kuna siku nyingine, wanafunzi walikuwa wakijisomea usiku, mara wakavamiwa na wahuni hao na walipotakiwa watoe kompyuta, simu na fedha na pale inapotokea hawakuwa navyo ama kuwabishia, basi wanajeruhiwa kwa mapanga.”

“Hiyo ni kweli kabisa, dada zetu wanabakwa sana tu ila hawasemi kwa kuogopa aibu katika jamii na hata taarifa zinapofikishwa polisi tunaishia kupewa RB tu halafu tunaambiwa watafuatilia.”

“Hawa watu si kwamba ni wageni, wanafahamika na hata maeneo yao wanayofanyia uharamia huo yanafahamika... Ukweli wanatunyima uhuru kabisa na tumesharipoti polisi lakini hakuna kinachoendelea. Tumeporwa zaidi ya kompyuta ndogo 300, kinachotuuma zaidi, hawa wezi wanafahamika wanapokaa na polisi inawaangalia.”

Wanafunzi wengine
Baadhi ya wanafunzi hao wanaoishi Kigamboni walidai kuwa wanaishi katika mazingira hatarishi kwani wakati mwingine uporaji hufanyika kweupe saa 11 jioni.

Maeneo yaliyotajwa kuwa ni hatari na wakazi wa Kigamboni ambayo wenyeji hulazimika kuyapita kabla ya saa 12:00 jioni ni Midizini, Minazi Mikinda, Mnara wa Rada, Kisimani na Serengeti.

Mwanachuo mwingine ambaye aliomba jina lake lihifadhiwe alisema: “Tofauti za kimaisha baina yetu ndiyo zinazosababisha chuki kuwa wanachuo wanaringa na kujiona wenye hadhi za juu ndiyo maana wanafanyiwa vitendo hivyo.

Wakazi nao wanena
Baadhi ya wakazi wa Kigamboni walisema kuwa mji huo ambao umepangwa kuwa wa kitalii sasa si salama.

Mmoja wa wakazi hao ambaye pia aliomba jina lake lisiandikwe gazetini alisema inapofika saa moja usiku, vitendo hivyo vya uporaji wa kutumia mapanga huanza na kuongeza kwamba kinachowasikitisha ni Jeshi la Polisi kufumbia macho vitendo hivyo.
Mwingine alisema wamekuwa wakipata usingizi wa shaka kutokana na kujawa hofu kuwa muda wowote wanaweza kuvamiwa na kuporwa.HABARI ZAIDI BONYEZA HAPA>>>


JIUNGE NA EDMO BLOG SASA

Usipitwe!! Jiunge nasi kupitia Facebook,Twitter na Instagram ili kupata habari zote za town! Usikose kujiunga na Youtube kuangalia video zote kali kutoka Edmo Blog Pekee!, kujiunga bonyeza hapa>>>Youtube

Tupe Maoni Yako lakini Usiandike Matusi



 
© Copyright EDMO BLOG | Designed By Peruzibongo