UKOSEFU WA DIWANI KATA YA BASHNET NI CHANGAMOTO

 
Serikali imeombwa kuharakisha uchaguzi mdogo wa udiwani wa kata  ya Bashnet iliopo wilaya ya Babati mkoani Manyara  ili waweze kumpata diwani atakayesimamia maendeleo katika kata yao.
 
 Wakiongea  na waandishi wa habari wakazi  wa kata hiyo  walisema  kuwa hivi sasa hawana diwani baada ya hivi karibuni aliyekuwa diwani wao Laurent Tara kuhama chama cha NCCR-Mageuzi na kuhamia Chadema hivyo kupoteza udiwani wake.
 
 Aidha walibainisha kuwa  kwa vile Tara alikuwa diwani wao kwa tiketi ya NCCR-Mageuzi tangu mwaka 2000 hadi Desemba 17 mwaka jana,wanatarajia kumchagua tena kupitia Chadema kwani amewaletea maendeleo makubwa ikiwemo suala zima la elimu.
 
 Naye mwenyekiti wa Halmashauri ya wilaya ya Babati Vijijini Nicodemus Tarmo amethibitisha kupokea barua ya Tara kujiuzulu nafasi ya udiwani baada ya kuhama NCCR-Mageuzi hivyo kupoteza sifa ya kuwa diwani.
 
 Alisema kuwa wameshaandika barua kwenye ofisi ya Waziri Mkuu ili kuwajulisha kwamba kata ya Bashnet hivi sasa haina diwani baada ya Tara kujitoa kwenye chama kilichompa ridhaa ya kuongoza wananchi.
 Alibainisha kuwa  suala la kufanyika kwa uchaguzi mdogo wa kujaza nafasi ya kumpata diwani wa kata hiyo linasubiri utaratibu kutoka Tume ya Taifa ya uchaguzi baada ya kupata barua kutoka ofisi ya Waziri Mkuu. 
 
 Naye mmoja kati ya wakazi hao Abraham Mlundi alieleza kuwa  tangu Tara awe diwani wao amefanikiwa kusimamia ujenzi wa shule tano za sekondari na shule 13 za msingi hivyo kufanya kata hiyo kuwa na sekondari nyingi zaidi katika mkoa huo.
 
Alisema kuwa  Tara ni diwani ambaye amejitahidi kuleta maendeleo kwenye kata hiyo hivyo wanaiomba Serikali iharakishe uchaguzi ili wapate mwakilishi kwani hivi sasa wamebakiwa na diwani wa viti maalum Angela Pius.
 
 Kwa upande wake Mchungaji Wemaeli Sarwat wa kanisa la Pentekoste Bashnet alieleza kuwa  kata hiyo itakuwa na pengo lisiloweza kuzibika baada ya Tara kujiuzulu kwani alikuwa anajulikana kwa jina la bwana maendeleo.
 
 Noberk Lucas ambaye alikuwa Mwenyekiti wa kijiji cha Guse (CCM) alisema  kuwa  Tara ameacha mambo mengi ya maendeleo ya kukumbukwa ikiwemo kilimo bora na kupigania haki za binadamu kwa kutoa elimu ya uraia.
 
 “Pia alishiriki kufanya mageuzi ya kilimo kwa kuwapa mbegu ya viazi mviringo kutoka Rongai mkoani Kilimanjaro na badala ya kupata magunia sita wakawa wanavuna magunia 25 hadi 30 kwa ekari moja,” alisisitiza Lucas.


JIUNGE NA EDMO BLOG SASA

Usipitwe!! Jiunge nasi kupitia Facebook,Twitter na Instagram ili kupata habari zote za town! Usikose kujiunga na Youtube kuangalia video zote kali kutoka Edmo Blog Pekee!, kujiunga bonyeza hapa>>>Youtube

Tupe Maoni Yako lakini Usiandike Matusi



 
© Copyright EDMO BLOG | Designed By Peruzibongo