MKUU WA WILAYA YA MAKETE ATOA MAFANIKIO YA SERIKALI YA AWAMU YA NNE WILAYANI HUMO



Mkuu wa wilaya ya Makete Mh. Josephine Matiro akisoma taarifa ya mafanikio ya serikali ya awamu ya nne katika Ukumbi wa halmashauri ya wilaya hiyo

Wajumbe wakifuatilia kwa makini taarifa hiyo ya mkuu wa wilaya
 
Wilaya ya Makete hii leo imetoa taarifa ya mafanikio ya serikali ya awamu ya nne tangu mwaka 2005-2012 kwa kuelezea mafanikio hayo katika sekta mbalimbali kufuatia agizo la waziri mkuu Mizengo Pinda alilolitoa kwa wakuu wa mikoa na wilaya kufanya hivyo





Akisoma mafanikio hayo mbele ya viongozi wa serikali na binafsi pamoja na wananchi, Mkuu wa wilaya ya Makete mh. Josephine Matiro amesema kuwa wilaya imepiga hatua katika nyanja mbalimbali zikiwemo elimu, kilimo, afya, maji, na maliasili





Akizungumzia sekta ya kilimo mh. Matiro amesema wilaya imekuwa na ongezeko la mavuno kutoka tani 74,219 mwaka 2005 hadi 145,436 mwaka 2012 ikiwa ni ongezeko la asilimia 95 huku matumizi ya pembejeo za kilimo yakichangia ongezeko hilo





Amesema matumizi hayo ya pembejeo yanatumika katika shughuli zote za kilimo ikiwemo mahindi na viazi





Pamoja na mambo mengine katika sekta hiyo pia serikali imefanikiwa kujenga mifereji mitatu ya umwagiliaji kwani tangu mwaka 2005 mifereji hiyo haikuwepo ambayo ni mifereji ya Mfumbi, Luwumbu na Ikuwo na miradi hiyo imegharimu zaidi ya shilingi milioni 430





Kwa upande wa sekta ya afya mkuu huyo wa wilaya amesema kumekuwa na ongezeko la vituo vya kutolea huduma za afya hadi kufikia 41, hospitali 3 vituo vya afya 5 na zahanati 33 huku vituo vya kutolea huduma za unasihi na upimaji zikiongezeka kutoka vituo 3 mwaka 2005 hadi 15 mwaka 2012





Amesema idadi ya watu wanaopima virusi vya ukimwi kwa hiari imeongezeka kutoka 109 sawa na asilimia 18 mwaka 2005 hadi 21,417 mwaka 2012





Akishukuru kwa niaba ya waalikwa waliofika kusikiliza taarifa hiyo, Mwenyekiti wa halmashauri ya wilaya ya Makete Mh. Daniel Okoka ameshukuru kwa utaratibu huo ulioanzishwa na serikali huku akiikubali taarifa hiyo na kusema ndiyo hali halisi





“sisi kama halmashauri tunakubaliana na taarifa hiyo iliyosomwa na mkuu wa wilaya na imelenga karibu sekta zote hivyo ni wajibu wetu kuzidi kufanya kazi ili taarifa ijayo ikija iwe nzuri zaidi ya hapa” alisema Okoka





Amesema wilaya imepiga hatua ya kimaendeleo huku akitolea mfano kuwa wilaya ya makete imejitahidi kujenga madaraja ya zege kwenye mito mikubwa iliyopo wilayani humo tofauti na wilaya nyingine jambo linalopelekea TANROADS kuipongeza wilaya kwenye vikao mbalimbali





“Ukiangalia kwenye mito mikubwa yote tumejenga madaraja ya zege kwani ni ukweli usiopingika kuwa kuna wilaya zinatumia madaraja ya miti hadi sasa, kwa kweli hili ni jambo la kujivunia tena sana” alisema Okoka





Pia kwenye kikao hicho mkuu wa wilaya alitoa fursa ya wadau mbalimbali walioshiriki kuchangia maoni ama kuuliza maswali kuhusiana na mafanikio hayo, huku wadau hao wakitoa maoni yao pamoja na ushauri huku wengine wakiuliza maswali ambayo yalipatiwa majibu kutoka kwa wataalamu waliohudhuria kikao hicho





Kutokana na agizo hilo la waziri mkuu taarifa ya mafanikio ya serikali ya awamu ya nne itakuwa ikisomwa kwa wananchi kila baada ya miezi minne


JIUNGE NA EDMO BLOG SASA

Usipitwe!! Jiunge nasi kupitia Facebook,Twitter na Instagram ili kupata habari zote za town! Usikose kujiunga na Youtube kuangalia video zote kali kutoka Edmo Blog Pekee!, kujiunga bonyeza hapa>>>Youtube

Tupe Maoni Yako lakini Usiandike Matusi



 
© Copyright EDMO BLOG | Designed By Peruzibongo