MH JOHN MNYIKA:SERA YA MAJIMBO NI SIRI YA MAENDELEO YA NCHI

Na John J.Mnyika
Mwaka 2007 miaka miwili baada ya uchaguzi wa mwaka 2005 palijitokeza mjadala kuhusu sera ya majimbo. Mwaka 2012 ikiwa ni miaka miwili tena toka uchaguzi wa mwaka 2010 pameibuka kwa mara nyingine mjadala kuhusu sera ya majimbo kufuatia maandamano ya wananchi wa Mtwara juu ya madai ya gesi. Waziri wa Nishati na Madini Prof. Sospter Muhongo amenukuliwa na gazeti moja tarehe 29 Disemba 2012 akiponda sera ya majimbo ya Chama Cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA) kuwa ni mbovu na haitumiki kokote duniani; kauli ambayo haina ukweli kama nitavyoeleza katika makala hii.  Amedai madai ya rasilimali za wananchi wa eneo hayana msingi na kuwaita wote wenye kujenga hoja hiyo kuwa wanataka kuigawa nchi vipande vipande, majibu ambayo ni mwendelezo wa propaganda chafu.

Prof. Muhongo badala ya kujibu hoja za waandamanaji na wananchi wa Mtwara ameamua kuibua ‘vioja’ vya kuishambulia CHADEMA na sera yake ya majimbo. Wakati hata kwa sera za CCM na serikali ya sasa, maandamano ya wananchi wa Mtwara kutaka majibu toka  kuhusu manufaa ya miradi ya gesi  asili inayotoka katika maeneo yao ni matokeo ya madai ya ufisadi wa baadhi ya viongozi na udhaifu wa Serikali katika kuushirikisha umma katika michakato ya maamuzi ya  kisera na kitaasisi kuhusu rasilimali na miradi muhimu ya maendeleo. Aidha, ni matokeo pia Bunge kutokuisimamia kikamilifu Serikali kwa niaba ya wananchi kwa mujibu wa ibara ya 63 ya katiba wakati serikali inapoacha kufafanua masuala yanayohojiwa na wabunge na inapokwepa kutekeleza maazimio ya Bunge kuhusu sekta ya nishati ikiwemo sekta ndogo ya gesi asili.

Nashauri Rais Jakaya Kikwete apuuze majibu ya Prof. Muhongo na  atumie hotuba yake kwa taifa ya mwishoni mwezi huu wa Disemba 2012 kueleza kwa umma undani wa miradi husika ya gesi asili  na manufaa yake kwa wananchi wa maeneo tajwa na nchi kwa ujumla; hatua ambayo alipaswa kuifanya tarehe 8 Novemba 2012 wakati wa uzinduzi wa mradi husika.
Nikirudi kwenye madai potofu ya Prof. Muhongo kuwa sera ya majimbo ni mbovu, haitumiki kokote duniani na itaigawa nchi vipande vipande, nirejee majibu yangu ya mwaka 2007 kwa wasome na wanasiasa wenye mtizamo kama wake. Nikumbushe tu kwamba madai potofu kama hayo yalishika kasi sana wakati wa uchaguzi mkuu 2005 kwa vijembe vya majukwaani. Hoja kuu ya kufahamu ni kwamba chimbuko la sera ya majimbo nchini ni falsafa ya CHADEMA ya nguvu ya umma. Kwani umma ndio unapaswa kuwa na mamlaka lakini pia umma ndio unapaswa kunufaika na rasilimali za nchi. Falsafa hii imeelezwa vizuri katika ibara ya 3 ya katiba ya CHADEMA ambayo nashauri Prof. Muhongo na wote wenye mtizamo kama wake waisome na kuielewa.


JIUNGE NA EDMO BLOG SASA

Usipitwe!! Jiunge nasi kupitia Facebook,Twitter na Instagram ili kupata habari zote za town! Usikose kujiunga na Youtube kuangalia video zote kali kutoka Edmo Blog Pekee!, kujiunga bonyeza hapa>>>Youtube

Tupe Maoni Yako lakini Usiandike Matusi



 
© Copyright EDMO BLOG | Designed By Peruzibongo