BANDARI SASA KUKATWA MISHAHARA KUFIDIA UPOTEVU MALI ZA WATEJA

Dk Harrison Mwakyembe.
Baada ya kuwang’oa vigogo wa bandarini kwa ubadhirifu na matumizi mabaya ya madaraka, sasa Waziri wa Uchukuzi, Dk Harrison Mwakyembe, amewageukia wafanyakazi.
 
Dk Mwakyembe ameagiza wafanyakazi watakaohusika na upotevu wa mali za wateja wote kuanzia mwezi ujao, walipe fidia ya mali hizo, kupitia mishahara na posho zao.
 
Akizungumza juzi mbele ya Kamati ya Bunge ya Miundombinu, Dk Mwakyembe alisema ili kupunguza wizi mdogo na udokozi bandarini, wateja  watakaopotelewa na vifaa vyao bandarini, Mamlaka ya Usimamizi wa Bandari (TPA), itawajibika kufidia.
 
Fidia hiyo kwa mujibu wa Dk Mwakyembe, itatokana na    bajeti ya TPA na pengo la bajeti hiyo, litazibwa  kwa kuwakata mishahara na posho wafanyakazi wote waliokuwepo kwenye eneo la tukio wakati udokozi ukitokea.  
 
Katika taarifa yake hiyo ambayo gazeti hili linayo, Dk Mwakyembe, alisema kutokana na hatua ambazo Wizara hiyo imechukua dhidi ya vitendo vya ubadhirifu kwa baadhi ya viongozi wa mamlaka hiyo, tayari mafanikio yameanza kupatikana katika kipindi cha muda mfupi.
 
“Kuanzia Mei, mwaka jana hadi leo (juzi) hakuna kontena lililodaiwa kuibwa au kupotea. Hata hivyo udokozi kwenye mizigo pamoja na magari, bado unaendelea na mchezo huu tutaukomesha.
 
“Kuanzia mwezi ujao wateja watakaopotelewa na vifaa watalipwa fidia na wahusika kukatwa mishahara na posho zao,” alisema.
 
Alisema ufanisi wa upakuaji mizigo ambao umekuwa tatizo kwa miaka mingi bandarini hapo, umerejea kwa kasi ambapo muda wa kusubiri meli tangu inapoingia nchini mpaka inaondoka, umepungua kutoka siku 21 hadi siku 14 na sasa ni siku saba tu.
 
“Tayari nchi za Rwanda, Burundi na Uganda zimetuma mawaziri wake wa Uchukuzi nchini kuelezea utayari wao sasa kutumia Bandari ya Dar es Salaam,” alisema Dk Mwakyembe.


JIUNGE NA EDMO BLOG SASA

Usipitwe!! Jiunge nasi kupitia Facebook,Twitter na Instagram ili kupata habari zote za town! Usikose kujiunga na Youtube kuangalia video zote kali kutoka Edmo Blog Pekee!, kujiunga bonyeza hapa>>>Youtube

Tupe Maoni Yako lakini Usiandike Matusi



 
© Copyright EDMO BLOG | Designed By Peruzibongo