SUMATRA YAWABANA WAMILIKI WA MAGARI MADOGO MKOANI MARA KUHUSU NAULI


KONDA AKIWA KWENYE DALADALA
 
Tarime
 
Mamlaka ya udhibiti wa usafiri wa majini na nchi kavu SUMATRA mkoani Mara, imewaagiza wamiliki wa magari madogo ya abiria wilayani Tarime, kuzingatia nauli elekezi zilizopangwa na mamlaka hiyo na kuonya kuwa wamiliki watakaobainika kuendelea kutoza nauli ambazo ni kinyume na viwango hivyo watachukuliwa hatua kali za kisheria ikiwemo kufungiwa leseni zao.
 
Agizo hilo limetolewa mjini Tarime na Afisa mfawidhi wa Sumatra mkoa wa Mara, Kapteni Michael Rogers,wakati wa zoezi la ukaguzi wa magari ya abiria yanayotoa huduma kati ya wilaya ya Tarime na miji ya Musoma na Mugumu pamoja na maeneo ya Sirari, Nyamongo na Shirati katika wilaya ya Rorya mkoani Mara.
 
Kaimu kamanda wa kikosi cha usalama barabarani Kanda Maalum ya Tarime/ Rorya, mkaguzi wa polisi Charles Ntenga, amewashauri wananchi kutoa ushirikiano kwa askari wa usalama barabarani kuhusu magari yanayoendelea kutoza nauli kubwa tofauti na viwango vya Sumatra, huku akiwaonya wale watakaojaribu kuchezea sheria.
 
Katibu wa chama cha wamiliki wa magari madogo ya abiria wilayani Tarime Kazimoto Kabila, pamoja na baadhi ya wadau wa usafirishaji na abiria wamesema SUMATRA inapaswa kufikiria upya viwango vya nauli kutokana na kupanda kwa bei za mafuta, vipuri vya magari na kuharibika kwa miundombinu ya barabara ili waweze kuendesha biashara zao kwa faida.


JIUNGE NA EDMO BLOG SASA

Usipitwe!! Jiunge nasi kupitia Facebook,Twitter na Instagram ili kupata habari zote za town! Usikose kujiunga na Youtube kuangalia video zote kali kutoka Edmo Blog Pekee!, kujiunga bonyeza hapa>>>Youtube

Tupe Maoni Yako lakini Usiandike Matusi



 
© Copyright EDMO BLOG | Designed By Peruzibongo