NEWS ALERT: MWILI WA MHARIRI WA JAMBO LEO WAHIFADHIWA KATIKA HOSPITALI YA TAIFA MUHIMBILI


 Mhariri Mtendaji wa kampuni ya Free Media ambayo inachapisha magazeti ya Tanzania Daima na Sayari, Absalom Kibanda akimpa pole Mkurugenzi wa Jambo Concepts, Juma Pinto kufuatia kifo cha Mhariri Mkuu wa gazeti la Jambo Leo, Willy Edward kilichotokea mkoani Morogoro usiku wa kuamkia leo. (Picha zote na Mpiga Picha wa Habari Mseto Blog).
 Mkurugenzi wa Jambo Concepts, Juma Pinto  akilia kwa uchungu baada ya kuona gari lililokuwa limebeba mwili wa aliyekuwa Mhariri Mkuu wa Jambo Leo marehemu Willy Edward likiingiza mwili wa marehemu katika chumba cha kuhifadhia maiti katika hospitali ya Taifa ya Muhimbili jijini Dar
 Mhariri wa gazeti la Tanzania Daima Jumapili, Salehe Mohamed (kushoto), Mhariri wa Habari Mtanzania, Mwandishi wa Michezo Tanzania Daima, Ruhazi Ruhazi na Frank Balile wa gazeti la Super Star
Baadhi ya Wahariri na waandishi waandamizi wakiushusha mwili wa marehemu ili kuhifadhiwa katika hospitali ya Taifa muhimbili mara baada ya kuwasili kutokea Morogoro.
 Mwili wa marehemu ukiingizwa katika chumba cha kuhifadhia maiti.
Baadhi ya wafanyakazi wenzake wakiwa muhimbili wakati mwili wa marehemu ukihifadhiwa.
Baadhi ya waombolezaji wakiwa nyumbani kwa aliyekuwa Mhariri Mkuu wa Jambo Leo marehemu Willy Edward Murahati jijini Dar es Salaam. Wa tatu kushoto ni mke wa marehemu, Rehemaheri Willy Edward. (Picha zote na Mpiga Picha wa Habari Mseto Blog).
Mtoto wa marehemu Willy Edward, Careen Willy Edward.

DAR ES SALAAM, Tanzania
Mhariri   Mkuu wa gazeti la kila siku la Jambo Leo Willy Edward,  amefariki dunia usiku wa kuamkia leo akiwa mjini Morogoro alikoenda kuhudhuria semina ya siku moja iliyoandaliwa na ofisi ya Taifa ya Takwimu (NBS) na kuwashirikisha wahariri wa vyombo mbali mbali vya habari.
Kwa mujibu wa Kulwa Karedia ambaye ni mhariri wa gazeti la Mtanzania,alisema marehemu kabla ya kufikwa na umauti alikuwa ni mzima wa afya na kwamba aliwaaga kuwa anaenda  kuwaona watoto wake wanaoishi mkoani humo ambapo alikaa huko mpaka saa 6:30. Marehemu ameacha mke na watoto watatu.

Alisema muda wa kurudi katika hoteli aliyofikia ulipowadia Marehemu alimwita dereva wa Piki Piki ili amchukue na kwamba usafiri huo ulipofika hakuweza kuipanda kwani alipotoka nje na kutembea kwa hatua kama sita kabla ya kuifikia piki piki alianguka.
Karedia aliongeza kuwa ndugu zake walimkimbiza hosipitali na baada ya vipimo vya daktari ikabainika kuwa alikwisha fariki dunia.
Kaka wa Marehemu aliyejitambulisha kwa jina la Denis Ongiri, alisema wanatarajia kumzika marehemu  katika mji wa Mugumu Wilayani Serengeti.
Alisema kwa sasa Msiba upo nyumbani kwa kaka yake eneo la Mburahati NHC na kwamba taarifa ya lini mwili utasafirishwa zitatolewa baada ya ndugu kukutana na kutoa uamuzi wa pamoja.
“Suala hili limekuwa la ghafla sana ninachoweza kusema kwa sasa ni kwamba tutaenda kumzika wilayani Serengeti katika mji wa Mugumu,tunaomba ushirikiano wa watu wote katika hili kuanzia sasa mpka safari nyake ya mwisho”alisema Ongiri kwa huzuni.
Marehemu Willy Edward (kulia) enzi za uhai wake akiwa na Rais Jakaya Kikwete.

Na Edson Kamukara

“WILLY  twende zetu Dar, achana na Martin Malera, maana yeye huku Morogoro ni kwao amefika, hawezi kuondoka leo”.

Sikujua kama hayo ndiyo yalikuwa maneno yangu ya mwisho kwa kaka, rafiki na mwana tasnia wa habari, Willy Edward, ambaye nilikuwa naye jana mjini Morogoro kwenye semina ya siku moja kwa wahariri, iliyoandaliwa na Ofisi ya Taifa ya Takwimu (NBS).

Nasema sikujua kwa kuwa niliyasema kwa utani wakati tulipokuwa tukiagana na wenzangu, ndipo nikamsogelea Willy akiwa amekaa meza moja na mhaririri wa Tanzania Daima Jumatano, Martin Malera na James Range wa kituo cha televisheni cha Startv, nikiwaaga na kuwauliza kama wanaondoka kurejea Dar es Salaam.

Willy alinijulisha kuwa anabaki na ataondoka kesho yake akimaanisha Jumapili ya jana na wakati huo wote kwa pamoja na Malera walikuwa wakitutania kuwa tunakimbilia wapi kwanini hatutaki kulala Morogoro?

Ndipo nikamtania Willy nikisema twende, achana na Malera maana yeye ni mwenyeji wa mkoani humo, hivyo amefika hawezi kuondoka…(tukacheka) na kupeana mikono kisha tukaondoka na Range, Saleha Mohamedi (Mhariri wa Tanzania Daima Jumapili) na David Ramadhan (Chanel ten) na hivyo kumuacha Willy.

Kwa muda wote tuliokuwa naye kwenye semina hiyo, alionekana mchangamfu na kwa bahati nzuri tulikaa jirani na hivyo tulipata muda mrefu wa kuzungumza mambo mengi.

Nilipatwa na mshangao leo alfajiri baada ya kupokea simu ya Mhariri wangu Mtendaji, Absalom Kibanda, akiniuliza kama nina taarifa za kufariki kwa Willy Edward, kwa vile alidhani nami nililala Morogoro.

Nilinyanyuka ghafla kitandani, kwa ghafla nikakumbuka miongoni mwa wahariri waliyobakia kule, alikuwemo pia Kulwa Karedia wa Mtanzania na hivyo nikampigia simu kuhakikisha taarifa hiyo kama ni kweli.
Karedia baada ya kupokea simu yangu, aliniambia kwa sauti ya kunyong’onyea akisema, “Kamanda, Willy Edward hatunaye tena, nimejaribu kukupigia lakini simu yako nimekuwa siipati”.
Nilijikaza kumsikiliza Karedia huku nikibubujikwa na machozi, akanieleza kuwa Willy alikwenda kuwaona watoto wake na alikuwa huko hadi saa sita usiku, na kisha alimwita dereva wa pikipiki afike kumchukua kwa lengo la kurejea katika hoteli alikokuwa amefikia.
Lakini baada ya kutoka nje, kabla ya kupanda pikipiki alidai anasikia kizunguzungu na kisha alianguka.Wenzake walijitahidi kumkimbiza hosipitali lakini walipofika na kufanyiwa vipimo daktari aligundua tayari alikuwa ameshafariki dunia.
Hivyo ndivyo alivyozimika ghafla Willy Edward, ambaye mashabiki wa michezo watamkumbuka daima kama mpenzi wa mpira wa miguu na zaidi shabiki wa kutupwa wa Klabu ya Yanga kwa hapa nchini na Arsenal kwa timu za nje.
Pia Willy alipenda sana muziki wa dansi, ule wa zamani na huu wa kisasa, akiwa mshirika wa karibu wa bendi ya Twanga Pepeta, ambayo amefanya nayo kazi pia kwa muda kadhaa.
Nilimfahu Willy kwa ukaribu zaidi kuanzia 2009 tulipoanza kufanya kazi pamoja katika gazeti la Jambo Leo, tukiwa waandishi waanzilishi wakati huo yeye akiwa mhariri wa michezo.
Licha ya kwamba amefanya kazi katika vyombo vya habari tofauti lakini kwa muda mrefu, binafsi nilibahatika kufanya naye kazi katika gazeti la Jambo Leo na hata baada ya kuhamia Tanzania Daima, tumeendelea kuwa karibu.
Kwa muda wote wa miaka miwili na miezi mitatu niliyokaa naye Jambo Leo, nilimfahamu kwa undani na kutambua kuwa alikuwa mpole, mtaratibu na mkimya, aliyependa kusikiliza na kujifunza zaidi kabla ya kutenda au kuzungumza.
Willy alikuwa mchangamfu, mwepesi wa kuelekeza na mwenye kupenda ushirikiano na watu wengine. Alikaripia na kuonesha hasira pale ambapo ililazika kufanya hivyo lakini haikuwa hulka yake.
Pamoja na kubadilishwa nafasi kutoka mhariri wa michezo kuwa habari na kisha Mhariri Mkuu wa Jambo Leo, Willy alibakia kuwa yule yule mwenye silika ya upole na ushirikishaji wa wenzake asiyependa kujivuna.
Willy alipenda kukuza lugha ya Kiswahili kupitia tasnia ya habari, na katika kufanya hivyo kila mara alipenda kufanya kazi akiwa na kamusi ya Kiswahili pembeni, akichukua baadhi ya maneno na kuyatumia kwenye gazeti mara kwa mara kama misamiati mipya ambayo baadaye ilizoeleka.
Yako mengi ya kuandika kumhusu Willy Edward, ambaye sasa ni marehemu lakini itoshe kusema kuwa tumepoteza mtu muhimu katika tasnia ya habari na fani nyingine kama michezo na muziki.

Mungu ametoa na ametwaa, jina lake lihimidiwe. Tunamwomba ailaze pema peponi roho ya mwenzetu Willy Edward Ogunde. Lakini kwangu itanichukua muda kumsahau kaka yangu huyo.
 NA HABARI MSETO BLOG


JIUNGE NA EDMO BLOG SASA

Usipitwe!! Jiunge nasi kupitia Facebook,Twitter na Instagram ili kupata habari zote za town! Usikose kujiunga na Youtube kuangalia video zote kali kutoka Edmo Blog Pekee!, kujiunga bonyeza hapa>>>Youtube

Tupe Maoni Yako lakini Usiandike Matusi



 
© Copyright EDMO BLOG | Designed By Peruzibongo