Mapigano yalizuka baada ya mechi.
Baraza la utawala wa kijeshi nchini Misri limetangaza siku tatu za maombolezo ya kitaifa baada ya watu wasiopungua 74 kuuwawa katika mapigano kati ya mashabiki wa timu pinzani katika mji wa Port Said.
Mamia kadhaa walijeruhiwa wakati mashapiki waliuvamia uwanja baada ya mechi kati ya timu mbili zinazoongoza kwenye ligi al-Masry na al-Ahly.
Mikutano ya dharura ya baraza la mawaziri pamoja na bunge imeitishwa.
Maandamano yamepangiwa kufanyika Alhamisi kulaani hatua ya polisi kutochukua hatua yoyote kuzima fujo hizo.
Mechi zote za ligi kuu nchini Misri zimeahirishwa kwa muda usiojulikana.
Mmoja wa mashabiki wa klabu ya al-Ahly ameiambia BBC kwamba mashabiki wenzake wataandamana kutoka makao makuu ya klabu hiyo mjini Cairo hadi katika afisi za wizara ya mambo ya ndani.
Na BBC