Atoa saa 24 askari wa TANAPA waliopiga wananchi wakamatwe

Mkuu wa Mkoa wa Mbeya, Juma Homera ametoa saa 24 kwa Jeshi la Polisi kuwamkamata askari wa TANAPA wanaodaiwa kuwapiga wananchi wa eneo la hifadhi wilayani Mbarali.

Hayo yamejiri kufuatia hoja aliyoiwasilisha Mbunge wa Jimbo la Mbarali, Fransis Mtega juu ya tukio hilo ambalo lilimfanya Waziri Mkuu, Kasimu Majaliwa kuiagiza Wizara ya Maliasili na Utalii na uongozi wa TANAPA kufika eneo husika mara moja na kushughulikia tatizo hilo.

“Kwenye hili la kupiga watu nimetoa maagizo kwa Kamanda wa Polisi wa Mkoa ahakikishe wale askari wote waliofanya kitendo hicho wakamatwe wapelekwe polisi na wafunguliwe kesi kama raia wengine, natoa saa 24 wawe wameshakamatwa, wachukuliwe hatua kama wahalifu wengine,” amesema.

Homera ameongeza kuwa Serikali haijawahi kutuma askari kupiga au kunyanyasa raia bali jukumu la askari ni kulinda raia na mali zake.

Wakizungumza kwa masikitiko, baadhi ya wananchi wa eneo hilo la hifadhi wameiomba Serikali kuwatengea eneo salama kwa ajili ya mifugo yao ili kuondokana na unyanyasaji wanaopitia kutoka kwa askari hao.

“Hamjatupatia eneo la kuweza kuishi na mifugo yetu lakini tunaambiwa kwamba sisi tuishi mifugo itoke, tunaomba tupate sehemu angalau tunaposubiri utaratibu wa Serikali, angalau mifugo yetu ibaki sehemu salama,” ameeleza mmoja wa wananchi.


JIUNGE NA EDMO BLOG SASA

Usipitwe!! Jiunge nasi kupitia Facebook,Twitter na Instagram ili kupata habari zote za town! Usikose kujiunga na Youtube kuangalia video zote kali kutoka Edmo Blog Pekee!, kujiunga bonyeza hapa>>>Youtube

Tupe Maoni Yako lakini Usiandike Matusi



 
© Copyright EDMO BLOG | Designed By Peruzibongo