Mkuu wa Usalama Barabarani Mkoa wa Iringa na Mrakibu wa Polisi, Mossi Ndozero amepiga marufuku watoto wadogo chini ya miaka tisa kupanda pikipiki wakiwa pekee yao kwani inahatarisha usalama wao pindi wanapokuwa kwenye pikipiki hizo.
Akizungumza na wazazi katika Shule ya Msingi Wambi iliyopo katika Halmashauri ya Mji Mafinga, Ndozero amesema watoto chini ya miaka tisa hawapaswi kupanda kwenye pikipiki wakiwa peke yao bila kuwa na mtu mzima kwa ajili ya usalama wao.
Amesema kuwa licha ya kuwepo kwa changamoto zetu za usafiri, pia Sheria ya Usalama Barabarani hairuhusu mtoto chini ya miaka hiyo kupanda pikipiki hizo kwani inahatarisha usalama wao kutokana na watoto hao kukosa uangalizi.
"Niwaombe wazazi kuacha tabia ya kuwapakia watoto kwenye pikipiki kwa sababu sheria ya usalama barabarani hairuhusu mtoto chini ya miaka tisa kupanda pikipiki na kama unampandisha basi lazima awe na mtu mzima wa kumuangalia," amesema Ndozero.
“Unampakia mtoto kwenye pikipiki halafu upepo unampuliza kisha anapata usingizi, anaweza kuondoka na kupoteza maisha. Hapo inakuwa hasara ni vizuri kumwangalia kwa umakini mkubwa watoto wetu ili wasipate madhara," amesema mkuu hiyo wa Polisi.