Pinda: Adhabu ya kifo ifutwe nchini

Hoja ya kufutwa kwa adhabu ya kunyongwa inazidi kupata nguvu, baada ya Waziri Mkuu mstaafu, Mizengo Pinda kuungana na wadau wengine kutaka adhabu hiyo ifutwe na badala yake iwe kifungo cha maisha.


Mapendekezo ya Pinda yanaungana na wadau mbalimbali, wakiwamo mawakili, watetezi wa haki za binadamu na Baraza la Makanisa ya Kipentekosti Tanzania (CPCT) ambao wameshauri kufutwa kwa adhabu hiyo.

Pinda alizungumzia adhabu hiyo alipozungumza na wanahabari, baada ya kutoka kuwasilisha maoni na mapendekezo yake kwa Tume ya Haki Jinai.

Tume hiyo iliundwa na Rais Samia Suluhu Hassan ili kuangalia na kumshauri jinsi ya kuboresha mfumo na taasisi zinazohusika na suala la haki jinai.

Pinda alisema adhabu hiyo inampa tabu, kwa kuwa ni kufanya kosa juu ya kosa, na kwamba hadhani kama inatibu tatizo.

“Mimi adhabu ya kunyongwa inanipa taabu, kwa sababu ni kweli ametoa roho ya mtu katika mazingira yake, kwa hiyo sasa ili tumkomeshe, tumnyonge. Ni kosa juu ya kosa. Sidhani kama inatibu ugonjwa huo,” alisema Pinda na kuongeza:

“Adhabu hizi mara nyingi hazina tija sana kwa maana ya kuwafanya watu wasifanye hayo. Kinyume chake ni mkiwa na utaratibu unaowatia matumaini, wanaweza wakaona kumbe jambo hili ukilifanya ni baya, kwa nini tusirudi tu kwenye adhabu ya maisha?”

Alisema hata hao wa adhabu ya maisha kama baada ya miaka fulani huwa wanatoka kwa msamaha na kurejea uraiani, mtu huyo hawezi tena kwenda kuua isipokuwa kama ni mgonjwa wa akili.

“Kikubwa mimi ni hilo tu kwamba unaua na wewe unauawa. Kwa hiyo waliangalie tu. Nchi nyingi zilishaiondoa,” alisema Pinda.

Alisisitiza jibu la muuaji si kumuua kwa sababu kiuhalisia halisaidii kupunguza wauaji.


JIUNGE NA EDMO BLOG SASA

Usipitwe!! Jiunge nasi kupitia Facebook,Twitter na Instagram ili kupata habari zote za town! Usikose kujiunga na Youtube kuangalia video zote kali kutoka Edmo Blog Pekee!, kujiunga bonyeza hapa>>>Youtube

Tupe Maoni Yako lakini Usiandike Matusi



 
© Copyright EDMO BLOG | Designed By Peruzibongo