Aliyezikwa arejea nyumbani akiwa hai, yabainika alizikwa mtu mwingine

Biashara ilisimama katika kitongoji duni cha Nairobi nchini Kenya Ijumaa jioni, wakati mwanamume anayeaminika kuzikwa katika Kaunti ya Kisii wiki tatu zilizopita kurejea.


Hili liliwashangaza jamaa, waendesha boda boda, na wakazi wengine waliokuwa wameongoza waombolezaji katika hafla ya mazishi ya Meshack Ondiek Nyambane. 


Mamia ya raia walijaa kwenye makao makuu ya polisi katika tarafa ya South B, wakitarajia kupata majibu kuhusiana na kujitokeza tena kwa mwanamume huyo, Nation Africa iliripoti. 


Maafisa hao wa polisi walikuwa na wakati mgumu kudhibiti umati huku wakaazi wakiwa na shauku ya kushuhudia kile walichokitaja kuwa miujiza.


Hali ya utulivu ilirejea wakati mkuu wa polisi wa Makadara Judith Nyongesa alipowasili baada ya kupigiwa simu na Mkuu wa Kituo cha South B Robert Mbui. Nyongesa alifichua kuwa Nyambane, mhudumu wa bodaboda, alikamatwa na kufungwa jela kwa kuwazuia madereva na watumiaji wengine wa barabara katikati mwa jiji mnamo Februari 14. 


Alikamatwa na askari wa kaunti na baadaye kupelekwa katika mahakama ya City Hall, ambapo alihukumiwa kifungo cha miezi miwili gerezani alipokiri kosa. Nyambane alikuwa na stakabadhi iliyoonesha alikuwa ametekeleza kosa hilo, alitumikia kifubgo chake jela na aliachiliwa katika jela y Ruiru. 


Alisema alikuwa ameachiliwa Ijumaa baada ya kukamilisha kifungo chake. Nyambane alikuwa amerejea kuanzisha tena kazi yake ya bodaboda kwenye barabara ya South B/ South C kabla ya kutiwa mbaroni.


Ni hapo ambapo familia ya Nyambane na marafiki walibaini walikuwa wamezika mwili usio wa wake. Hata hivyo, binamuye Nyambane, Paul Magara mwenye umri wa miaka 33 ambaye ni afisa wa gereza la Industrial Area alisema ndugu yao aliutambua mwili wa mhudumu huyo wa bodaboda. 


Magara alisema familia ilipiga ripoti kwa afisa wa polisi wa eneo lao kwamba jamaa yao alikuwa ametoweka ambapo mara moja alianza kusakwa kwa muda wa wiki moja. Kisha walimtaarifu mkewe ambaye alikuwa Saudi Arabia kuhusiana na kutoweka kwake. 


Baadaye makafani ya City iliwapigia simu kuwaarifi kuwa kulikuwepo na mwili uliopatikana katika bomba la maji taka. "Mwili ulikuwa katikma hali mbovu, ni kana kwamba ulikuwa umemwagiwa dutu. Kakake mkubwa aliutambua mwili," Magara alisema. Kennedy Magara, jamaa mwingine wa familia hiyo alisema walijitayarisha kwa siku mbili kuisafirisha maiti kwa mazishi. 


"Wahudumu wa bodaboda walijitokeza kumshughulikia mwenzao ili azikwe kiheshima huku hela zikichangwa apate kupumzishwa kwa haraka kutokana na hali mbaya ya mwili."


Aliongeza kuwa aliongoza kamati ya mazishi jijini Nairobi, na hafla hiyo ilifanyika katika kijiji cha Nyambaterere katika tarafa ya Nyacheki, kaunti ndogo ya Nyamache mnamo Machi 3. Mkewe Nyambane alisafiri kwa ndege kutoka Saudi Arabia kuungana na binti zao wawili kumzika. 


Kamanda Nyongesa alisema polisi wanaendelea na uchunguzi wa tukio hilo. "Nimewasiliana na mkuu wa polisi wa kaunti ndogo ya Nyamache ili taratibu za polisi zichukue mkondo wake. 


Ninawaomba wananchi wawe makini wakati wa kubaini maiti ili kuepuka makosa kama hayo," alisema.


Chanzo:tuko.co.ke


JIUNGE NA EDMO BLOG SASA

Usipitwe!! Jiunge nasi kupitia Facebook,Twitter na Instagram ili kupata habari zote za town! Usikose kujiunga na Youtube kuangalia video zote kali kutoka Edmo Blog Pekee!, kujiunga bonyeza hapa>>>Youtube

Tupe Maoni Yako lakini Usiandike Matusi



 
© Copyright EDMO BLOG | Designed By Peruzibongo