VIDEO: CCM Makete yataka wakandarasi wawili barabara moja, Mkurugenzi atoa Ufafanuzi

Serikali imeombwa kubadili wazo la kununua Taa za Barabarani katika Maeneo ya Tandala na Iwawa wilayani Makete mkoani Njombe badala yake Itumie fedha hizo kufanya matengenezo ya Barabara ya Kipengele Lupila ili kuboresha Uchumi wa wananchi wa eneo hilo.

 

Ombi hilo limetolewa hivi karibuni na Padri Sikrepa Mwamengele wa Parokia ya Sunji Lupila alipopewa nafasi ya kuzungumza na wananchi mbele ya Viongozi mbalimbali wa Dini na serikali katika Uwekaji wa Jiwe la msingi la Ujenzi wa Mradi wa Maji wa Mbalatse Lupombwe.

 

Katika kauli yake Padri Mwamengele amesema Ombi la kutoa fedha za kuweka taa hizo  lililotolewa kwa Rais Samia Suluhu Hasan alipofanya ziara wilayani Makete Agosti 9, 2022 anaona lisitishwe na gharama za kunulia taa hizo zielekezwe kufanya matengenezo ya Barabara ya Kipengele Lupila ili wananchi wasipate adha inayotokana na ubovu wa barabara hiyo hasa wakati wa masika.

 

Katika kuonesha suala la barabara hiyo kufanyiwa matengenezo hasa wakati huu msimu wa mvua ukiwa karibu, Mwenyekiti wa CCM wilaya ya Makete Clemence Ngajilo ameitaka serikali wilayani hapo kuhakikisha barabara hiyo inafanyiwa matengenezo mapema kabla mvua haziajaanza kunyesha kutokana na barabara hiyo kuwa tegemezi kwa wananchi wa ukanda huo wa kata za Lupila na Mbalatse

 

Mkurugenzi Mtendaji Halmashauri ya wilaya ya Makete Bw Wiliam Makufwe ametolea majibu ya serikali juu ya Barabara hiyo ambapo amesema tayari Mkandarasi amepatikana kwa ajili ya kuitengeneza na kwa sasa anaendelea na ujenzi wa barabara ya Ibaga na watakachokifanya ni kumhimiza ili awahi kuja kuitengeneza barabara ya Kipengele Lupila mapema kabla ya mvua kuanza kunyesha

 

Makufwe amesema kutokana na jiografia ya wilaya ya Makete, wakandarasi wengi hawajitokezi kwa wingi kuomba zabuni katika halmashauri hiyo, hivyo wamejipanga kununua seti ya mitambo itakayowasaidia wakandarasi hao katika shughuli zao ili kusiwe na visingizio.

 

Edibily Mgaya, na Augustino Msemwa  ni wananchi wa kata ya Mbalatse eneo ambalo barabara hiyo inapita, wamesema kipindi cha masika barabara hiyo haipitiki hali inayowapelekea kushindwa kufanya shughuli zao za kila siku hivyo wameiomba serikali kutekeleza ahadi zake badala ya kuendelea kuwahidi kila wakati pasina kutekeleza.


JIUNGE NA EDMO BLOG SASA

Usipitwe!! Jiunge nasi kupitia Facebook,Twitter na Instagram ili kupata habari zote za town! Usikose kujiunga na Youtube kuangalia video zote kali kutoka Edmo Blog Pekee!, kujiunga bonyeza hapa>>>Youtube

Tupe Maoni Yako lakini Usiandike Matusi



 
© Copyright EDMO BLOG | Designed By Peruzibongo