Mbunge wa Geita Vijijini Joseph Msukuma, amevitaka vyombo vya ulinzi na usalama kuacha tabia ya kuwazuia wananchi wanaounga mkono juhudi za Rais John Pombe Magufuli za kupambana na wezi wa raslimali za taifa ikiwemo madini.
Msukuma aliyasema hayo baada ya polisi katika wilaya ya kipolisi Msalala, kuzuia maandamano ya amani na mkutano wa hadhara yaliyoandaliwa na mbunge wa Msalala mkoani Shinyanga, juzi jumamosi katika eneo la Kakola.
Hata hivyo polisi walitoa idhini ya mkutano wa hadhara kufanyika katika uwanja wa Bugarama badala ya Kakola kwa madai kwamba walipata taarifa za uvunjifu wa amani katika eneo la Kakola.
Naye mbunge wa Msalala Ezekiel Maige alisema bado ataandaa mkutano mwingine utakaofanyika Kakola ili kutoa fursa ya wananchi wengi kujitokeza kutoa pongezi kwa Rais Magufuli pamoja na kero zao baada ya wengi wao kushindwa kufika katika mkutano wa jana kutokana na umbali wa kwenda Bugarama.
Alisema halmashauri ya Msalala inaidai migodi ya Buzwagi na Bulyanhulu takribani shilingi tilioni mbili ambazo atahakikisha zinalipwa ili kusaidia maendeleo ya jimbo lake ikiwemo ujenzi wa barabara ya lami ya Kahama-Geita.
Katika mkutano huo, bado kilio cha wakazi wa Kakola kilikuwa ni kuutaka mgoni wa Bulyanhulu kuwalipa fidia zao za ardhi na zile za baadhi ya wafanyakazi kuumia na kuachishwa kazi huku baadhi yao wakikumbushia machungu ya ndugu zao kufukiwa mashimoni wakati wakihamishwa ili kupisha shughuli za mgodi ambapo nao wanashinikiza kulipwa fidia.