Watuhumiwa hawa kumi wafikishwa mahakamani Kisutu

Watuhumiwa 10 wakiwemo raia wawili wa Guinea, wamefikishwa katika mahakama ya hakimu mkazi Kisutu, Dar es Salaam wakikabiliwa na mashitaka ya kujihusisha na mtandao wa uhalifu na kukutwa na meno ya Tembo yenye thamani ya sh bilioni 4.6. 

Washitakiwa hao wamesomewa mashitaka matatu chini ya sheria ya uhujumu uchumi na sheria ya uhifadhi wa wanyamapori ambapo walisomewa na jopo la mawakili wanne wa serikali, wakiongozwa na Paul Kadushi, mbele ya hakimu mkazi mkuu, Dk Yohana Yongolo. 

Katika mashitaka yao inadaiwa kuwa tarehe tofauti kati ya Aprili 6 na Juni 26, mwaka huu Dar es Salaam, kwa pamoja wanadaiwa kupanga, kuratibu, kusimamia na kufadhili mtandao wa uhalifu kwa kuuza, kupokea na kusafirisha nyara za serikali ambazo ni vipande 660 vya meno ya Tembo bila kuwa na kibali kutoka kwa mkurugenzi wa wanyamapori. 

Hakimu Yongolo amesema washitakiwa hawatakiwi kujibu mashitaka kwa kuwa mahakama hiyo haina mamlaka ya kusikiliza kesi hiyo isipokuwa mahakama kuu, ambapo upande wa jamhuri umedai upelelezi wa kesi hiyo bado haujakamilika na kuomba tarehe nyingine ya kutajwa. 

Kabla kesi hiyo hajahahirishwa mshitakiwa Victor alidai anaumwa kwasababu ya kupigwa wakati akiwa kwenye kituo cha polisi, hivyo aliiomba mahakama itoe maelekezo ili apewe matibabu hali iliyomlazimu hakimu Yongolo aliamuru mshitakiwa huyo apewe matatibu akiwa gerezani. 

Kesi hiyo imeahirishwa hadi Julai 28, mwaka huu na washitakiwa wamerudishwa rumande kwa kuwa mashitaka yanayowakabili hayana dhamana.

CHANZO: ITV


JIUNGE NA EDMO BLOG SASA

Usipitwe!! Jiunge nasi kupitia Facebook,Twitter na Instagram ili kupata habari zote za town! Usikose kujiunga na Youtube kuangalia video zote kali kutoka Edmo Blog Pekee!, kujiunga bonyeza hapa>>>Youtube

Tupe Maoni Yako lakini Usiandike Matusi



 
© Copyright 2025 EDMO BLOG | Designed By Peruzibongo