KATIBU
Mkuu wa CCM, Abdulrahman Kinana ameandika barua ya kujiuzulu nafasi
hiyo kwa Mwenyekiti mpya wa CCM, Rais John Magufuli, lakini Rais
amekataa barua yake hiyo.
Badala
yake, Rais Magufuli amemtaka Kinana na manaibu katibu wakuu wawili na
sekretarieti nzima ya chama hicho, kuendelea na kazi.
Hayo yalisemwa na Rais Magufuli wakati akitoa hotuba ya kushukuru wajumbe wa Mkutano Mkuu Malumu wa CCM, mjini hapa.
“Nimepata
barua ya Kinana ya kujiuzulu nafasi yake pamoja na wakuu wa idara za
sekretarieti. Nimeamua Kinana na sekretarieti yote waendelee kuwepo.
“Kama kutakuwa na haja baadaye nitaitisha kikao cha Halmashauri Kuu ya Taifa (NEC) na siyo leo,” alisema Magufuli, akiwatangazia wajumbe hao wa kikao cha Mkutano Mkuu, ambacho ni kikao cha juu cha chama.
Alisema
kwa kuwa mkutano huo ndiyo wenye uamuzi wa mwisho kuhusu masuala ya
chama, hivyo anawauliza wajumbe kama wamekubaliana na pendekezo lake
hilo la Sekretarieti ya chama iendelee.
“Nawauliza
wajumbe mnaafiki?” Ambapo wote kwa kauli moja walisema; “Ndiyo.”
Magufuli alisema kulikuwa na watu waliokuwa wamejipanga kuchukua nafasi
hizo za sekretarieti, lakini “sasa imekula kwao”. Hakutaja watu hao.
Akiongeza kuwa; “Nitaendelea
kuwa na Kinana na nina imani yeye na sekretarieti nzima watasimamia
vizuri mambo kadhaa niliyoagiza yasimamiwe haraka.”
Magufuli
alisema CCM ni chama cha aina yake duniani, kwa kuwa kila upande kuna
fursa ya ushauri kutoka kwa wazee wastaafu (huku akiwataja kwa majina),
jambo linalofanya kazi iliyo mbele yake kuwa nyepesi.