Ishu ya mauaji Utweve, Mkuu wa Wilaya atoa kauli, Wananchi Washangilia

Wananchi wa kijiji cha Utweve kata ya Ukwama wilayani Makete wameshauriwa kutosusia shughuli za maendeleo kijijini hapo na badala yake waendelee kuzifanya kama awali, wakati serikali ikishughulikia kero zao zinazowakabili

Kauli hiyo imetolewa Jana na Mkuu wa wilaya ya Makete Mh Veronica Kesi wakati alipofika kijijini hapo kusikiliza kero za wananchi ikiwemo baada ya wao kutangaza kugomea shughuli za maendeleo kwa madai ya kutoridhishwa na mwenendo wa shauri la kuuawa mtoto mmoja kijijini hapo na watuhumiwa wa mauaji hayo kupewa dhamana

Mh Kesi amesema anaungana na wananchi hao kuwapa pole kwa msiba huo uliowapata na kusema hoja zote zilizotolewa na wananchi katika mkutano huo amezichukua na kuahidi kwenda kuzifanyia kazi na wananchi kuona majibu kwa kuwa ziko hoja ambazo zipo ndani ya uwezo wake na nyingine zilizopo kwa upande wa mahakama watashirikiana na wataalamu wakiwemo wanasheria kuzitatua kisheria

Pia mkuu huyo amelaani mauaji hayo na kusema si vizuri mtu yeyote kujichukulia sheria mikononi na kusababisha kifo cha mwananchi yeyote


Aidha mkuu huyo amewaagiza viongozi wa kijiji hicho na kata ya Ukwama kutenga siku maalumu ya kusikiliza kero za wananchi ili zitatuliwe haraka iwezekanavyo kwa kuwa njia hiyo itasaidia kuimarisha kijiji hicho na kisonge mbele kimaendeleo


Katika mkutano huo Mkuu wa wilaya ametoa nafasi ya kusikiliza maoni ya wananchi kuhusiana na tukio la mauaji ya mtoto wa miaka 17 lililotokea kijijini hapo miezi miwili iliyopita
Mwanasheria wa wilaya ya Makete Bw. Godfrey Gogadi ametolea ufafanuzi wa baadhi ya hoja za wananchi ikiwemo kutojadili suala ambalo lipo mahakamani kwa kuwa sheria hairuhusu, na kwa kuwa suala la mauaji hayo lipo mahakamani ni vema wananchi wakawa na subira na kuiachia mahakama itende haki, na kwa kuwa malalamiko yao wameyafikisha kwa mkuu wa wilaya, atashirikiana na wataalamu wake ili suala hilo lifikie mwisho vizuri bila kuathiri chochote


JIUNGE NA EDMO BLOG SASA

Usipitwe!! Jiunge nasi kupitia Facebook,Twitter na Instagram ili kupata habari zote za town! Usikose kujiunga na Youtube kuangalia video zote kali kutoka Edmo Blog Pekee!, kujiunga bonyeza hapa>>>Youtube

Tupe Maoni Yako lakini Usiandike Matusi



 
© Copyright EDMO BLOG | Designed By Peruzibongo