Walimu 4 wakamatwa na polisi wakidaiwa kupigania mnofu wa kuku

WALIMU wanne wa sekondari Jumapili walijipata katika seli za polisi mjini Murang’a Kenya baada ya kupigana kwa kudaiwa kutofautiana kuhusu mlo wa kuku katika baa moja ya mji huo.
Walimu hao ambao walikuwa wakiburudika pamoja kwa vilewesho walikamatwa kwa madai ya kuvuruga amani ya umma waliporushiana makonde na kusababisha uharibifu wa mali katika baa hiyo.
Kwa mujibu wa afisa mpelelezi katika kisa hicho Bw Judah Muriuki, walimu hao wa kiume walitofautiana kuhusu mlo wa kuku; jogoo mmoja wa kilo nne.
“Shida ilitokea wakati mchuuzi wa kuku aliingia akitafuta wateja wa jogoo kadhaa aliokuwa nao. Alipofika katika meza ambayo waalimu hao
walikuwa, kukatokea kejeli za ni nani angeweza kumaliza kuku huyo akiwa peke yake,” akasema.
Mwalimu mmoja anasemekana kuwa alidai angeweza kumaliza jogoo huyo akiwa peke yake, bora tu iwe amekaangwa vizuri na atiwe supu vikombe viwili.
Kulingana na Bw Muriuki, wenzake mwalimu huyo walisema hakuna namna hilo lingewezekana.
“Ndipo mwalimu huyo aliwaagiza wenzake wanunue jogoo huyo aliyekuwa akiuzwa kwa Sh1,200 na ikiwa hataweza kummaliza kama alivyokuwa akidai, basi yeye mwenyewe angetoa Sh5,000 kama fidia kwao,” akasema afisa huyo wa polisi.
Inasemekana kuwa kuku huyo alichinjwa na akakatwa vipande kadhaa na akatayarishwa namna mwalimu huyo alikuwa ameagiza.
“Kutayarishwa, nyama ililetwa katika meza hiyo. Mwalimu aliyekuwa amedai angeimaliza akaanzana nayo. Akaanza na vipande vya miguu,
akaenda kwa kipapatio na kisha akachukua kipande kimoja cha mgongo,” akaarifu afisa huyo wa polisi.
Ni wakati walimu wenzake waliona kana kwamba mwenzao angeimaliza nyama hiyo ya kuku huyo ambapo waliirukia nyama hiyo na wakaanza kuibishania na hatimaye vita vya makonde na urushaji chupa ukatokea.
Hasara
Kwa mujibu wa Bw Muriuki, walimu wenzake walionelea wangeenda hasara ikiwa mwenzao angeikula nyama hiyo animalize peke yao ilihali wao ndio walikuwa wameinunua.
“Lakini ajabu ni kuwa baada ya kuwakamata, mwalimu huyo alidokeza kuwa hakuna uwezekano angeimaliza nyama hiyo na alikuwa anawaza jinsi ya kupata fedha za kuwalipa wenzake kwani alikuwa amelemewa katika kilo moja tu na kiasi kidogo juu yake,” akasema.
Hata hivyo, walimu hao waliachiliwa Jumatatu asubuhi bila ya mashtaka yoyote baada ya muungano wa walimu (KUPPET) tawi la Murang’a kuingilia kati.
Hata hivyo, duru za kuaminika ziliashiria kuwa walimu hao walitoa kitu kidogo cha kununua msamaha ndipo wakaachiliwa, jambo ambalo wote walikana.
“Hakuna pesa zozote zilitolewa na upande wowote. Tuliamua tu kuwasamehea ikizingatiwa kuwa walikuwa shereheni kama wanataaluma
lakini tofauti kidogo zikazuka,” akasema Bw Muriuki.


JIUNGE NA EDMO BLOG SASA

Usipitwe!! Jiunge nasi kupitia Facebook,Twitter na Instagram ili kupata habari zote za town! Usikose kujiunga na Youtube kuangalia video zote kali kutoka Edmo Blog Pekee!, kujiunga bonyeza hapa>>>Youtube

Tupe Maoni Yako lakini Usiandike Matusi



 
© Copyright EDMO BLOG | Designed By Peruzibongo