Wajawazito wa Kata ya Igale wilayani Mbeya,
wamelalamikia kufukuzwa na kunyimwa huduma kutoka kwa
baadhi ya wahudumu wa afya wa zahanati za vijiji kwa madai
wananuka kwa sababu ya kutooga.
Mwenyekiti wa Kituo cha Taarifa na Maarifa cha Mtandao wa
Jinsia Tanzania (TGNP) wa kata hiyo, Lyidia Sankemwa alisema
hayo alipowasilisha taarifa ya kero za wananchi alizopokea
kwenye kituo chake.
Sankemwa alisema wajawazito wa vijiji vya Itaga, Igale, Horongo, Izumbwe na Shongo, walifika kwenye kituo chake na kulalamika kuhusu kufukuzwa na
wahudumu wa afya “Tumepokea malalamiko mengi kutoka kwa wajawazito kuwa baadhi ya watoa huduma za afya
katika zahanati zetu wanawafukuza kwa madai kuwa wananuka na hatimaye kucheweleshewa
kupata huduma,” alidai Sankemwa.
Katibu wa Kituo hicho, Alfred Mwambugu alisema kutokana na tatizo hilo, baadhi ya wajawazito
wanakataa kwenda kupata huduma katika zahanati hizo kwa kuhofia kutolewa lugha chafu.
Akizungumzia malalamiko hayo, Ofisa Habari wa Halmashauri ya Wilaya ya Mbeya, Hamza Mwangomale alisema ameyapokea na kushawasiliana na mratibu wa afya kwa ajili ya kuandaa
kikao cha pamoja na watoa huduma za afya wa zahanati zinazotuhumiwa.
Ofisa Mtendaji wa Kata ya Igale, Alinanuswe Mwakamala alisema kata hiyo yenye vijiji vitano ina
zahanati nne ambazo hazikidhi mahitaji.
Alisema kata hiyo ina wakazi 11,800 wanaohudumiwa na zahanati nne na Kijiji cha Horongo
hakina zahanati, wakazi wake hulazimika kufuata huduma kwenye zahanati za vijiji vingine kwa
umbali wa kilomita tano.