Kesi ya kupinga matokeo ya uchaguzi ya Mbunge wa jimbo la Kinondoni Maulid Mtulia (CHADEMA) iliyofunguliwa na aliyekuwa Mbunge wa jimbo hilo, Idd Azzan imeshindwa kutolewa maamuzi hii leo kama ilivyokuwa imepangwa na mahakama kuu ya Tanzania.
Juma Nassoro ambaye ni wakili wa mshtakiwa Maulid Mtulia Mbunge wa Kinondoni amesema kuwa baada ya kesi hiyo kusikilizwa na Jaji Lugano Mwandamb kwa njia ya maandishi ilipangwa kutolewa maamuzi leo, ila kwa bahati mbaya jaji huyo hakuweza kufika mahakamani kutokana na kupangiwa kushughulikia kesi nyingine za uchaguzi mkoani Kilimanjaro.
Hata hivyo, Jaji huyo alimuomba msajili kumpanga jaji mwingine atakayeshughulikia hukumu hiyo. Mahakama iliamuru warudi tena kesho mahakamani kwa ajili ya kupangiwa tarehe nyingine.
Kwa upande wa Mbunge Mtulia anayekabiliwa na kesi hiyo ameeleza kusikitishwa na kilichotokea kwa kile aalichodai kuwa kesi hiyo haina madai ya msingi na hivyo mahakama ilistahili kuitupilia mbali badala ya kuendelea kuipiga kalenda.