Wananchi wa Lupalilo Makete waikataa taarifa ya mapato na matumizi ya kijiji

Wananchi wa kijiji cha Lupalilo kata ya Lupalilo wilayani Makete mkoani Njombe wamekataa kuipokea taarifa ya mapato na matumizi ya kijiji hicho ya Septemba hadi Desemba 2015

Wananchi hao wamefikia hatua hiyo baada ya kutokubaliana na matumizi ya shilingi 201,000 yaliyotumika kwa ajili ya kushughulikia kesi ya kifusi pamoja na wajumbe wa halmashauri hiyo kutumia zaidi ya shilingi laki tano kwa ajili ya kujilipa posho

Baada ya majadiliano ya muda mrefu kwenye mkutano wa kijiji wananchi walimuamuru mwenyekiti wa kijiji hicho ambaye baada ya muda alijiuzulu Bw. Victoni Sanga kuzirudisha fedha hizo na wakati kijiji kikiwasomea taarifa ya mapato na matumizi itakayofuata ambayo itasomwa mwezi Machi mwaka huu, fedha hizo ziwe zimerudi

“jamani hivi hawa wajumbe tuliwatuma wakagawane posho au wasimamie maendeleo ya kijiji chetu? Kwa kweli mwenyekiti mimi naona hawa wajumbe wa halmashauri ya kijiji wapo kujinufaisha, haiwezekani watumie zaidi ya laki tano kwa ajili ya posho tu hivi sisi tutaendelea lini jamani?” amesikika mwanamama mmoja akizungumza kwenye mkutano huo bila kutaja jina lake

Pamoja na maamuzi hayo ya wananchi kaimu Afisa Mtendaji wa kata hiyo Bw. Mwatima Mbiliyi amewaambia wananchi hao kuwa wajumbe wako sahihi kutumia kiasi hicho cha fedha kwa ajili ya posho kwa kuwa kosa ni la kwao wananchi kutopanga watumie shilingi ngapi kwa kila mjumbe katika vikao vyao

“Mimi nasema wajumbe wako sahihi kabisa kutumia kiasi hicho cha fedha, na tena msiwalaumu kwa kuwa kosa ni lenu wananchi hamkuwapangia watumie shilingi ngapi, sasa mnawalaumu kwa lipi? Japo mimi ni mgeni hapa Lupalilo lakini nimejifunza kitu, ili kuondokana na yote haya mnatakiwa muwapangie kila mjumbe apewe posho ya shilingi ngapi kwa kila kikao wanachokifanya” amesema Mbilinyi

Naye diwani wa kata hiyo Mh. Imani Mbilinyi amesema wananchi hao wapange kiwango cha kulipwa wajumbe huku akitolea mfano katika kijiji cha Kisinga ambacho kipo katika kata yake kuwa wamepanga kila mjumbe alipwe shilingi 2,000 kwa kila kikao wanachokaa, jambo ambao limeondoa malumbano katika kijiji hicho
 Mwananchi akielezea sababu za kukataa taarifa hiyo

Kaimu Afisa mtendaji wa kata ya Lupalilo Bw. Mbilinyi akisisitiza jambo kwa wananchi baada ya taarifa hiyo kukataliwa


JIUNGE NA EDMO BLOG SASA

Usipitwe!! Jiunge nasi kupitia Facebook,Twitter na Instagram ili kupata habari zote za town! Usikose kujiunga na Youtube kuangalia video zote kali kutoka Edmo Blog Pekee!, kujiunga bonyeza hapa>>>Youtube

Tupe Maoni Yako lakini Usiandike Matusi



 
© Copyright EDMO BLOG | Designed By Peruzibongo