POLISI Mkoani Mbeya, inawashikilia watu wawili kwa tuhuma za kupatikana na nyara za serikali ambazo ni pembe za mnyama Faru kilo tano pamoja na vipande vinne vya mawe vinavyodhaniwa ni madini yenye uzito wa kilo moja.
Pembe hizo, zinadaiwa zinathamani ya zaidi ya milioni 80 wakati thamani ya mawe hayo yanayodhaniwa kuwa ni ya madini haijajulikana wala ni aina gani ya madini.
Akizungumza na waandishi wa habari ofisini kwake jana, Kamanda wa Polisi wa Mkoa wa Mbeya, Ahmed Msangi, alisema watuhumiwa hao walikamatwa jana majira ya saa nane za mchana katika mpaka wa Kasumulu unaotenganisha nchi mbili ya Tanzania na Malawi.
Aliwataja watuhumiwa hao kuwa ni Arquemides Joao Mahanjane akiwa na paspoti namba 13AF5838 na Henriques Benditor Assuba akiwa na pasipoti yenye namba AF24132 wote wakazi wa Maputo nchini Mozambique.
Akielezea tukio hilo, Kamanda Msangi alisema kuwa watuhumiwa hao wakiwa kwenye gari namba za usajili ABL 860 MC aina ya Toyota Hilux Vigo Double Cabin, wakiwa katika harakati za kuhakiki pasipoti, baadhi ya maofisa wa polisi na idara nyingine waliwatilia shaka na hivyo kufanya upekuzi.
Alisema, katika upekuzi huo walifanikiwa kukuta nyara hizo mbili za pembe za Faru zenye thamani ya shilingi milioni 82, 692,000 na vipande vine vya mawe yanayodhaniwa ni madini ambayo bado hayajajulikana aina yake.
Aidha, watuhumiwa hao walifikishwa katika mahakama ya Wilaya ya Kyela mbele ya hakimu mfawidhi Roda Martini na kusomewa mashitaka na kupatikana na hatia hiyo na kufungwa jela miaka nane kwa kosa la kupatikana na nyara za serikali kinyume cha sheria.
| Kamanda wa Polisi Mkoa wa Mbeya ACP Ahmed Msangi akionesha Pembe za Faru kwa Waandishi wa Habari(Picha na David Nyembe wa Fahari News) |
| Waandishi wa Habari wakimsikiliza kwa makini Kamanda |
| Kamanda wa Polisi Mkoa wa Mbeya ACP Ahmed Msangi akiangalia sehemu ambayo walikuwa wameficha Pembe hizo za Faru. |
| Mwonekano wa Sehemu walipokuwa wameficha Pembe hizo za Faru kwenye Gari. |