Katika hali isiokuwa ya kawaida mfanyabishara mmoja amejikuta akiambulia kichapo kutoka kwa wananchi wenye hasira kali baada ya kuchoma matairi zaidi ya 400 katikati ya makazi ya wananchi katika kijiji cha Kilimahewa kata ya Mbuyuni manispaa kwa lengo la kutaka kupata mabaki ya nyaya ili kuuza kama chuma chakavu.
Mtu huyo aliyejulikana kwa majina ya Mosha Ramadhani amejikuta akiwa mikononi mwa kamati ya ulinzi na usalama ya kijiji baada ya kupata kichapo ambapo amekiri kufanya makosa ya kuchoma matairi katika makazi ya watu kwa nguvu baada ya kukatazwa na wananchi kwa kisingizio cha hali ngumu ya maisha na alifanya hivyo ili kupata nyaya za kuuza aendeshe maisha.
Kwa upande wao wananchi wa kijiji cha kilima hewa akiwemo mwenyekiti wa kijiji hicho Sajigwa Mwakiruma wamelaani kitendo hicho ikiwa ni pamoja na mwenyekiti walichukua hatua kumpeleka mtuhumiwa katika kituo cha polisi kwa tuhuma za kuharibu mazingira.