Mkimbizi kutoka Burundi afa kimaajabu....Azikwa kwa tahadhari


Habari na picha na Editha Karlo, wa Globu ya Jamii Kigoma



MTU mmoja ambaye ni raia kutoka nchi ya Burundi amefariki usiku wa kuamkia leo katika hospitali ya Kigoma  kwa ugonjwa usiojulikana. 



Mgonjwa huyo amezikwa leo jioni  kwa tahadhari zote zihusuzo magonjwa ya kuambukizwa.



Nguo, vitanda, mashuka na vitu vyake vyote alivyokuwa akitumia wakati wa uhai wake vimechomwa moto mara tu baada ya mwili wake kuzikwa eneo la Masanga nje kidogo ya mji wa Kigoma.



(Picha zinaonesha hatua mbalimbali toka mwili wa marehemu ulipoondolewa na wataalamu waliovaa mavazi maalumu hadi mazikoni).



Akiongea na mtandao huu daktari wa wakimbizi  kutoka shirika la kusafirisha wakimbizi  kwenda nje ya nchi  (IOM) Dkt.  Beda amesema kuwa marehemu ameishi  katika kambi ya wakimbizi ya Nyalugusu Wilayani Kasulu kwa muda wa miaka mitatu  yeye pamoja na familia yake.



Dkt Beda amesema kuwa marehemu Buchumi Joely  (39) alifika Kigoma mwezi uliopita akiwa yeye pamoja familia yake kwa ajili ya kusafirishwa na shirika la IOM kwenda marekani.

DK Beda alisema kuwa marehemu alianza  kuugua tarehe 31 ya mwezi uliopita kwa kutokwa na damu sehemu mbalimbali za mwili wake kama mdomoni, kwenye fizi na machoni.

"Ilipofika tarehe juzi Agosti  8 hali yake ilizidi kuwa mbaya ndipo uongozi ulipoamua kumpeleka katika hospital ya mkoa maweni kwaajili ya matibabu zaidi" alisema Dkt Beda.




Naye Kaimu mganga mkuu wa hospital ya nkoa wa kigoma Dkt Shija Ganai amethibitishia mtandao huu kuwa walimpokea mgonjwa huyo na kumlaza katika wodi namba 8 ya Grade One.



Alisema kuwa usiku wa kuamkia leo hali ya mgonjwa ilizidi kuwa mbaya na damu zilizidi kuongezeka, na walipompima maralia  alikuwa na joto la kawaida la nyuzijoto 36.




Dkt. Ganai ameeleza kuwa  ilipofika alfajiri ya kuamkia leo mgonjwa huyo alifariki dunia. Amesema  kwamba mpaka sasa  bado haijadhibitishwa kama mgonjwa huyo amekufa kwa ugonjwa wa  ebola japo alikuwa na dalili zote za ugonjwa huo.



"Tumeshatuma sampo ya damu  maabara kuu ya Taifa kwa ajili vipimo ili tujue ni ugonjwa gani uliomuuwa"alisema Dkt huyo.



Aliongezea kuwa hivi sasa madaktari, manesi pamoja na ndugu wote waliokuwa wanamuhudumia mgonjwa hivi sasa wapo chini ya uangalizi maalumu wa madaktari kwa muda wa siku 21.


JIUNGE NA EDMO BLOG SASA

Usipitwe!! Jiunge nasi kupitia Facebook,Twitter na Instagram ili kupata habari zote za town! Usikose kujiunga na Youtube kuangalia video zote kali kutoka Edmo Blog Pekee!, kujiunga bonyeza hapa>>>Youtube

Tupe Maoni Yako lakini Usiandike Matusi



 
© Copyright EDMO BLOG | Designed By Peruzibongo