Zoezi la uchukuaji fomu za kuwania Urais kuelekea Uchaguzi kuu wa mwezi Oktoba mwaka huu linazidi kuendelea katika ofisi za tume ya taifa ya uchaguzi, kufuatia Mpeperusha bendera ya Chama Cha Kijamii CCK, kukabidhiwa fomu hizo mapema leo.
Mpeperusha bendera huyo wa CCK katika uchaguzi huo wa baadaye mwaka huu Dokta GEOFREY MALISA, akizungumza baada ya kukabidhiwa fomu hizo, ameahidi chama chake kufanya kampeni za kiungwana zitakazojikita katika utulivu na msisitizo mkubwa ukiwa ni katika amani.
Katika hatua nyingine, Mgombea huyo hakuambatana na mgombea mwenza kama ilivyozoeleka, hali iliyolazimu chama hicho kutoa maelezo kwa waandishi wa habari waliotaka kufahamu nini sababu yake, lakini pamoja na sababu nyingine, Katibu Mkuu wake RENATUS MUHABI, ambaye pia alikuwa ni dereva wa mgombea Urais wa chama hicho, aliwataka waandishi wa habari kutokariri kwani CCK wana utaratibu wao waliojipangia.
CCK kinakuwa chama cha saba kuchukua fomu hizo na kesho chama cha URA kinatarajiwa kufikisha idadi ya vyama vinane kwa mujibu wa ratiba ya tume ya uchaguzi.