MMOJA wa makada 37 wa Chama Cha Mapinduzi (CCM), waliokuwa wakiwania kuteuliwa kugombea Urais kwa tiketi ya chama hicho, Amos Robart Siyantemi ameomba kujumuishwa katika kampeni za kumnadi John Magufuli kwenye uchaguzi mkuu wa Oktoba mwaka huu.
Katika mkutano wake na wanahabari jijini Dar es Salaam leo, Siyantemi alimuomba Mwenyekiti wa Taifa wa CCM, Dkt. Jakaya Mrisho Kikwete, Makamu wake Philip Mangula na Katibu Mkuu, Abdulrahman Kinana kumshirikisha katika timu ya kumnadi mgombea huyo, kwani hivyo ndivyo alivyowaahidi wananchi wakati akitangaza nia ya kuomba nafasi hiyo.
“Naiomba Kamati Kuu inishirikishe kwenye timu ya mgombea wetu, ninamwomba pia mgombea wetu John Pombe Magufuli afahamu kuwa kwa sababu ya ugumu wa itifaki katika kumuona, naomba anijumuishe katika timu ya kampeni. Hii yote ni kuonyesha kuwa ndani ya chama chetu bado kuna mshikamano mkubwa miongoni mwa wanachama.”
