Mbunge wa Kigoma kaskazini Mh.Zitto Kabwe ametangaza rasmi kutogombea tena ubunge katika jimbo hilo baada ya
uchaguzi mkuu wa Oktoba mwaka huu, huku akiwashukuru wananchi wa jimbo
lake kwa kumpa dhamana ya kuwawakilisha bungeni kwa kipindi cha miaka 10
licha ya kukutana na vikwazo vingi.
Akiongea na wapiga kura wake hao Zitto amesema kwa kipindi chote
akiwa mbunge alijitahidi kwa kadri alivyoweza kutetea si tu maslahi kwa
watu wa jimbo lake bali kwa taifa zima kwa ujumla na kwamba ataendelea kufanya hivyo kama raia ili kuondoa kila aina ya ufisadi na kutumia rasilimali za nchi kuondoa umasikini, ujinga na maradhi.
Baadhi ya mambo ambayo Mh.Zitto ameyataja kuwa anajisifia kuyafanya
yawezekane katika jimbo lake kuwa ni pamoja na kufikisha umeme katika
vijiji 16, wananchi wa jimbo lake kujiunga na mifuko ya hifadhi ya
jamii, kuboresha huduma za afya, kuanzisha miradi ya bandari na soko
kubwa katika kijiji cha Kagunga.