'Kikombe’ spesheli kinavyowasaidia wasichana kujikinga hedhi

Kikombe cha hedhiJOTO ni jingi na vumbi si haba katika Shule ya Upili ya PAG Huruma, Nairobi kutokana na wanafunzi wanaocheza uwanjani.
Kuwepo wa wageni katika shule hii kunavutia kwa muda umati mkubwa wa wanafunzi wa shule ya msingi inayopakana na shule hii.

Katika upande mmoja, baadhi ya wanafunzi, wavulana kwa wasichana, wameketi na wanaonekana kujadiliana, labda masomo yao, huku wale wa shule ya msingi wakiendelea kucheza mchangani bila kujali.

Dakika chache baadaye, kengele inakiriza kuashiria wakati wa kwenda nyumbani kwa wanafunzi wa shule ya msingi na wakati wa kuendelea na masomo ya kibinafsi kwa wanafunzi wa sekondari.

Lakini kwa kundi la wanafunzi wa kike wa shule hii, umewadia wakati wa kupokea mafundisho ila si ya kawaida waliozoea darasani.

Hata hivyo baadhi ya istilahi wanazozisikia wakati wa mafunzo haya wamekumbana nazo katika somo la Baolojia kwani ni mafunzo yanayohusu usafi na afya ya mfumo wa uzazi.

Darasa wanakosomea halina mwangaza wa kutosha na joto ni jingi lakini hali hiyo haiwazui kumakinika ili kufaidika kutokana na mafunzo hayo ya bure.

Baada ya kufahamiana, Rachael Ouko, mwalimu wao kwa wakati huu, kutoka shirika lisilo la kiserikali la Femme International, anaanza kikao kwa kuwauliza wanafunzi wanachofahamu kuhusiana na miili yao na changamoto zinazowakabili kama wasichana.

Anapokea majibu tofauti ila hakuna anayegusia donda ndugu kuhusu matatizo wanayokumbana nayo wanapokuwa kwenye hedhi haswa njia za kujikinga ambazo ni changamoto kuu inayowakabili maelfu ya wasichana kote nchini. Lakini Benta Oyugi, mkufunzi mwingine katika kikao hiki anawakumbusha hayo.
Hiki ndicho kiini cha mafunzo ya leo, anaeleza Bi Ouko, ingawa wasichana wanapokea mafunzo zaidi kuhusu usafi wa miili yao na ugonjwa wa saratani ya kina mama.
Binti huyu anawavutia wasichana hao kwa kuchomoa na kuwaonyesha makaratasi mawili yaliyochorwa mfumo wa uzazi wa kina mama ambayo anadhamiria kutumia kutoa mafunzo yake.

Gharama ya sodo
Wasichana wote walio katika darasa hili wametoka katika mtaa wa Mathare na Huruma ambako familia nyingi zinaishi katika hali ya umaskini mwingi na huenda mafundisho na msaada watakaopokea kuwa ya manufaa makubwa.
Kulingana na utafiti, idadi kubwa ya wasichana wanaoishi katika mitaa ya mabanda hawawezi kumudu gharama ya kununua sodo.
Takriban asilimia 65 ya wanawake na wasichana nchini hawawezi kumudu gharama hii, suala ambalo limepelekea wanawake na wasichana kutumia njia zingine kujikinga hedhi kila mwezi.
Njia hizi ni pamoja na kutumia vipande vya nguo, makaratasi (ya vitabu na shashi), manyoya, godoro, majani na njia zingine zilizo na athari mbaya ya kiafya.
“Changamoto kubwa kwa wanawake na wasichana wanaoishi katika mitaa hii ni kwamba hawawezi kumudu gharama ya sodo kila mwezi na ndiposa kuna haja ya kutafuta njia mbadala za kuwasaidia. Idadi kubwa hawaelewi athari za kutumia baadhi ya njia hizi,” asema Bi Ouko.
Asilimia kubwa ya wasichana katika vitongoji duni katika miji tofauti nchini na mashambani hushiriki ngono ili kupata pesa za kujikimu kimaisha ikiwemo kununua sodo kulingana na utafiti.
Ikizingatiwa kuwa pakiti moja ya sodo hununuliwa kati ya Sh60 na Sh80, bei ambayo kwa baadhi ya wanawake hasa wasio na mapato makubwa ya kifedha, kuna haja ya kuibua njia mpya za kuwapunguzia gharama wanawake, aeleza.
Na ndiposa shirika la Femme International likishirikiana na Kampuni ya Ruby Cup limekuwa likitoa bure vikombe maalum- vikombe vya hedhi, kwa wasichana na kina mama katika vitongoji duni jijini Nairobi, Kisumu na Mombasa ili kuwasaidia wakati wa hedhi.
Vikombe hivi kwa kiingereza 'menstrual cups’ vimewapunguzia gharama kubwa walionufaika kutokana na mradi huo ulioanzishwa mwaka wa 2012.
“Nilianza kutumia kikombe nikiwa kidato cha pili. Kimenisaidia sana kwa sababu kimeniondolea gharama ya kununua sodo kila mwezi. Sasa naweka akiba pesa ya hizo,” aeleza Judith Atieno, mkazi wa Huruma.
Kila mwaka, msichana mmoja ana uwezo wa kutumia zaidi ya sodo 200 wakati wa hedhi, kumaanisha analazimika kutumia pakiti kadha, ingawa kuna aina ya sodo ambazo zinaweza kuoshwa na kuvaliwa tena.

Muda wa kudumu
Kulingana na Maxie Mathiessen mmoja wa waanzilishi wa Ruby Cup, kikombe hicho kilichotengenezwa na silikoni inayotumiwa katika matibabu kina uwezo wa kudumu miaka kumi.
Hii inamaanisha kuwa kwa muda huo wote, mtumiaji hatahitaji kununua sodo, jambo linalowapunguzia gharama ya maisha watumiaji.
“Kinaweza kutumiwa kwa masaa kumi na mawili. Hii inamaanisha kuwa mwanafunzi anaweza kwenda shuleni bila kuwa na wasiwasi wa kuchafua vazi lake,” asema Bi Ouko.
Kwa sababu hii wasichana waliobaleghe wanaweza kuendelea na masomo yao bila kubabaika au kushiriki katika ngono ya kulipwa ili kupata pesa za kununua sodo, asema Amaia Arranz, Afisa Mkuu Mtendaji wa Ruby Cup, Afrika Mashariki.
Kikombe cha hedhi ni Sh1,800 humu nchini na kinauzwa katika baadhi ya maduka ya rejareja na maduka ya madawa kwa wale wanahitaji kukitumia.
Utafiti umebaini kuwa wasichana wengi hasa kutoka familia maskini huacha shule wanapovunja ungo. Hii ni kutokana na changamoto zinazowapata wakati huo wa maisha ikiwemo hofu ya kuchekelewa shuleni.
Bi Atieno alisomeshwa na amezoea kukitumia kikombe hiki ambacho kimekuwa sehemu ya maisha yake. Hata hivyo mamia ya wasichana hawana ufahamu sio tu kuhusiana na matumizi ya sodo bali pia afya ya uzazi na miili yao.
Hivyo mafunzo yanayotolewa siku hii ni muhimu sana kwa wanafunzi na watumiaji wa vikombe, “Lazima kina mama na wasichana wafunzwe jinsi ya kutumia kikombe hiki,” asema Dkt Caroline Kabiru, mmoja wa watafiti waliofanya uchunguzi kuhusiana matumizi ya vikombe vya hedhi kutoka Kituo cha Utafiti wa Watu Afrika (APHRC) nchini.
Kikombe hiki 'huvaliwa’ au kutiwa ndani ya njia ya uzazi mwanzoni mwa hedhi na kuna utaratibu maalum wa kukitumia, aeleza Bi Ouko wakati wa mafunzo hayo.
“Hedhi hutona ndani mpaka kikombe kinajaa au kinafikia sehemu fulani wakati ambapo mtumiaji anaweza kukitoa na kumwaga damu kwa choo,” asema Bi Ouko. Aliwaonyesha wasichana hao wa vidato vya pili na tatu utaratibu wa kuweka na kutoa bila kutatizika.
“Kinaweza kuvaliwa kwa masaa 12. Mtumiaji akitoa na kumwaga damu anafaa kukiosha halafu anakitia ndani tena ingawa sio lazima kukiosha,” aeleza Bi Ouko.
Anaeleza kuwa wanawake wanaweza kutumia karatasi ya shashi kupangusa kikombe chenyewe au wanaweza kukitumia tena kilivyo, aeleza.
Kulingana na Dkt Kabiru, uchunguzi umeonyesha kuwa kikombe hiki hakina madhara yoyote ya kiafya ila mtumiaji anapaswa kunawa mikono kabla ya kukirejesha ndani. Usafi ni kitu cha maana sana ili kuzima hatari ya kupata maambukizi ya maradhi. Anaeleza mtumiaji anafaa vile vile kunawa mikono baada ya kukitoa.

Kuhifadhi
Baada ya hedhi kuisha huwa kinachemshwa kwa dakika tano, sio kwa sufuria ya kupikia, lakini ndani ya bakuli ya alumini iliyotengewa kazi hiyo.
Shirika la Femme International huwapa wasichana ufadhili wa kikombe hicho, sabuni, bakuli na taulo ya kujipangusa mikono baada ya kunawa.
“Kikombe hiki husaidia wasichana kuweka siri wakati wa hedhi kila mwezi na pia huwasaidia kukaa wakiwa wasafi,” asema Dkt Kabiru.
“Ni bora kikombe hiki kuliko kufua vitambaa na kikasaidia wasichana wengi sana nchini ingawa sio kifaa cha ajabu sana. Kinawapa wasichana nafasi ya kuchagua watakachotumia kujikinga,” aongeza.
Lakini kwa wasichana wanaotoka kwa familia maskini, kikombe hiki ni mwokozi kwani zaidi ya kuwa kinawapunguzia hofu na aibu ya kila mwezi, kinawakinga kutokana na athari za umaskini kama vile kushiriki ngono ya kulipwa na kuwapunguzia wazazi wao gharama ya maisha.
“Kuna athari kubwa sana kwa wasichana ya kutokuwa na uwezo wa kujikinga hedhi vyema kwa vile ni ukiukaji wa haki zao. Ni kuwafedhehesha na kuwatesa,” limesema shirika la Hanshep katika tovuti yake.
Mamia ya wasichana wa shule za msingi na sekondari kutoka Mathare, Kibera, Kawangware, Dagoretti, Kisumu na Mombasa wamefaidika kutokana na msaada huo.
swahilihub@ke.nationmedia.com


JIUNGE NA EDMO BLOG SASA

Usipitwe!! Jiunge nasi kupitia Facebook,Twitter na Instagram ili kupata habari zote za town! Usikose kujiunga na Youtube kuangalia video zote kali kutoka Edmo Blog Pekee!, kujiunga bonyeza hapa>>>Youtube

Tupe Maoni Yako lakini Usiandike Matusi



 
© Copyright EDMO BLOG | Designed By Peruzibongo