Chama cha demokrasia na maendeleo Chadema mkoani Rukwa kimeshinda kwa
kishindo kwenye uchaguzi wa serikali za mitaa, uliofanyika jana kwenye
kata tano za manispaa ya Sumbawanga, kwa kushinda viti 38 kati ya viti
vya mitaa 44 vilivyokuwa vikipiganiwa kwenye uchaguzi huo, huku chama
cha mapinduzi kikiambulia viti vitano tu, na kimoja kikisubiri uchaguzi
kurudiwa baada ya wagombea kulingana kwa kura.
Akitoa matokeo hayo mjini Sumbawanga msimamizi mkuu wa uchaguzi huo
Bw Hamid Njovu, amesema uchaguzi huo ulikuwa ukifanyika kwa upya kabisa
kwenye kata tatu baada ya kuvurugika Desemba 14, mwaka uliopita, na
huku kwenye kata mbili za Izia na Sumbawanga asilia ukirudiwa katika
mtaa mmojammoja kuchagua mwenyekiti wa mtaa husika, na kwamba uchaguzi
huo umefanyika katika mazingira ya amani kabisa.
Akiongea nasi mwenyekiti wa Chadema wa mkoa wa Rukwa Bw Zeno
Nkoswe, amesema ushindi huo wa kishindo ni ishara njema kwa chama chake
kufanya vyema kwenye uchaguzi mkuu ujao, kwa kushinda viti vingi kwenye
ngazi za udiwani na ubunge, na hata rais ajaye kupatikana mwaka huu
kutoka kwenye chama hicho.
Kufanyika kwa uchaguzi huo kunafuatia kuingia kwa dosari kubwa
katika uchaguzi wa serikali za mitaa, uliofanyika nchini desemba 14,
mwaka uliopita.