ASKOFU AWAPASHA WANAOUA ALBINO....ATOA UJUMBE MZITO KWAO

WATU wanaojihusisha na mauaji ya albino kwa lengo la kusaka vyeo au utajiri, wameonywa waache tabia hiyo mara moja kwa kuwa Mungu anawaona na kuchukizwa na vitendo vyao.

Aidha, wametakiwa kutambua kuwa vitendo wanavyovifanya si tu vinaukwaza utawala wa duniani na kuleta maumivu kwa wanajamii, bali vinawafanya wajifungie milango ya mbinguni, kwa sababu, inafunguliwa kwa wenye matendo mema pekee na si wauaji.

Hayo yalisemwa na Askofu wa jimbo la Rulenge, Mhashamu Severin Niwemugizi wakati wa mahubiri kwenye ibada ya maziko ya aliyekuwa Askofu mstaafu wa Kanisa Katoliki, jimbo la Tunduru-Masasi, Mhashamu Askofu Magnus Mwalunyungu (85) aliyefariki hivi karibuni.

Askofu Niwemugizi, amesema kukatisha maisha ya mwingine, au kumtia kilema mtu mwingine ni dhambi ambayo binadamu anaweza kukwepa adhabu yake hapa duniani tu kwa kujificha asionekane, lakini akakamatwa na Mwenyezi Mungu na kuhukumiwa kwenye moto wa milele, siku ya hukumu yake itakapofika.

Askofu Niwemugizi alisema, njia zote hizo ovu zinazotumiwa na wanadamu kupanda kifedha na utawala zitaendelea kuwa mbwembwe tu za duniani, lakini mafanikio ya kweli na halali yatatokana na watu kujituma kufanya kazi kwa bidii, huku wakilindana na kusaidiana kwa upendo.

“Unamfanyia binadamu mwenzako ukatili na kuamini kuwa huonekani machoni pa watu, unamkata na kuondoa viungo vya mtoto mdogo mwenye ulemavu wa ngozi na kuvitumia kwa mambo yako ya kujiinua, kwa sababu mtoto huyo hawezi kujipigania na kukushitaki, ewe mwanadamu, acha kufanya hivyo kwa kuwa Mungu anakuona”.

“…Kila anayefanya ukatili huo atambue kuwa anaukana ufalme wa mbinguni. Ninafahamu kuwa wanaofanya hivyo ni wanajamii wenzetu wenye dini, walio batizwa kama ni wakristo, na wenye akili timamu zinazotosha kuwafanya watambue jema na baya.

Ni watu wenye makusudi na roho mbaya, ambao humkana Mungu na kutafuta kujikweza kwa njia hizo zisizofaa,” Askofu Niwemugizi alisema.


JIUNGE NA EDMO BLOG SASA

Usipitwe!! Jiunge nasi kupitia Facebook,Twitter na Instagram ili kupata habari zote za town! Usikose kujiunga na Youtube kuangalia video zote kali kutoka Edmo Blog Pekee!, kujiunga bonyeza hapa>>>Youtube

Tupe Maoni Yako lakini Usiandike Matusi



 
© Copyright EDMO BLOG | Designed By Peruzibongo