WAZEE WATAKA MAZURI YALIYOFANYWA NA SERIKALI YATAJWE

Pancras Ndejembi MWENYEKITI mstaafu wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) Mkoa wa Dodoma, Pancras Ndejembi ametaka mazuri yaliyofanywa na serikali ambayo ni mengi yatangazwe.

Alisema hayo wakati wa mkutano uliowakutanisha Baraza la Wazee wa CCM Mkoa wa Dodoma na Mkuu wa Mkoa wa Dodoma, Chiku Gallawa.

“Mazuri ya Serikali ni mengi sana ni lazima yasemwe Serikali ya Chama Cha Mapinduzi (CCM) imefanya mengi mazuri lakini hayasemwi, ifike wakati mazuri ya Serikali lazima yasemwe. “Kama kuna mtu ambaye anadhani serikali haijafanya lolote katika kuwaletea wananchi wake maendeleo huyo atakuwa ana lake jambo ” alisema Ndejembi.

Mzee Ndejembi alisema serikali ya CCM imefanya mambo mengi makubwa na mazuri katika nchi hii, ambayo kila mtu anatakiwa kujivunia akitaja barabara kama moja ya mafanikio kutokana na mitandao yake kuunganisha mikoa hadi wilayani.

Mzee Ndejembi ambaye amewahi kushika nyadhifa mbalimbali katika kipindi cha uongozi wa Mwalimu Nyerere, anasema kukaa kimya watu wakiisimanga serikali ya CCM haijafanya kitu ni uwoga usiokuwa na msingi.

Alisema taifa hili limepiga maendeleo makubwa katika sekta ya elimu, afya, mawasiliano na demokrasia na hayo lazimwa yasemwe wazi.

Katika mkutano huo naye Balozi mstaafu, Job Lusinde amesema kuna mambo mengi yamefanywa na serikali na kila mtu anatakiwa kutambua hilo.

Lusinde ambaye aliwahi kuwa Waziri wa kwanza katika Baraza la Mawaziri wa serikali ya kwanza ya Tanganyika baada ya Uhuru mwaka 1961, alisema serikali ya CCM imefanya mengi ambayo yanatakiwa kupongezwa.

Mkuu wa Mkoa alisema kwamba watahakikisha wanatangaza mafanikio ya serikali mkoani hapa, kutokana na ukweli kuwa serikali imewekeza sana mkoani humo lakini mengi hayasemwi.

Anasema kama mkoa wamejipanga kutangaza mambo yote ambayo serikali imefanya mkoani Dodoma kupitia televisheni, redio na magazeti.

Mmoja wa wajumbe wa baraza hilo, Dk Bright Mbaga anasema serikali ya CCM inapaswa kupongezwa kwa maendeleo yaliyopo sasa nchini katika nyanja za elimu, afya, miundombinu na mengineyo.

Anasema licha ya mkoa kuwa na changamoto mbalimbali, lakini wajibu wa wazee ni kuhakikisha mambo yanakwenda vizuri.

Mzee Jumanne Gombati alisema Dodoma yenye bahati ya kuwa na vyuo vikuu vingi, lazima wataalamu wake washiriki kufanya utafiti kwa kutumia vyuo vyao ili ifike mahali changamoto hiyo imalizike.


JIUNGE NA EDMO BLOG SASA

Usipitwe!! Jiunge nasi kupitia Facebook,Twitter na Instagram ili kupata habari zote za town! Usikose kujiunga na Youtube kuangalia video zote kali kutoka Edmo Blog Pekee!, kujiunga bonyeza hapa>>>Youtube

Tupe Maoni Yako lakini Usiandike Matusi



 
© Copyright 2025 EDMO BLOG | Designed By Peruzibongo