Muungano wa wanafunzi umelaani sheria
mpya iliyopitishwa na uongozi wa chuo kikuu cha Zimbabwe ambayo inapiga
marufuku wanafunzi hao ‘kupigana mabusu’.
Taarifa iliyoandikwa na shirika la
utangazaji Uingereza BBC, imesema kiongozi wa muungano wa wanafunzi
Zimbabwe, Gilbert Mutubuki amesema wataungana kuipinga sheria hiyo
kandamizi inayowanyima uhuru na kuwafanya wanafunzi hao wa chuo kikuu
kulinganishwa na watoto wa chekechea.
Katika vipeperushi vilivyobandikwa
sehemu mbali mbali chuoni hapo, vimeandikwa amri kuwa yoyote
atakayekutwa katika mazingira ya kutatanisha kama vile kupigana mabusu
ama kufanya mapenzi hadharani ataadhibiwa vikali.
Vile vile sheria hiyo imekataza
wanafunzi kuwaingiza wenzao wa jinsia tofauti katika mabweni yao, pamoja
na kuleta marafiki zao katika eneo la chuo ambapo wamesema ni sheria
inayowanyima haki ya kujumuika na wenzao.
Wanafunzi wa vyuo vikuu nchini humo
wamekuwa wakipingana na serikali mara kwa mara, ambapo kwa sasa kiongozi
huyo wa wanafunzi amehimiza wanafunzi wenzake kuipinga sheria hiyo.