WATU sita wameaga dunia jijini Dar es Salaam wakiwemo raia wawili wa kigeni ambao wamekutwa wamekufa chumbani kwao na miili yao ikiwa haina jeraha lolote.
Kwa
mujibu wa taarifa za Jeshi la Polisi, raia wa Afrika ya Kusini, Roxxane
Hillier (27), aliyekuwa Meneja wa Mgahawa uitwao Water Front katika
Hoteli ya Slipway Masaki na rafiki yake wa kiume aitwaye Hylton William
aliyekuwa fundi wa boti maeneo ya Slipway walikutwa wamekufa wakiwa
katika chumba chao walichokuwa wamepanga katika Hoteli ya Slipway.
Inadaiwa
kwamba Hillier hakuonekana kazini kwa muda wa siku mbili na mara ya
mwisho kuonekana ilikuwa Oktoba 12 mwaka huu saa 4.00 ambapo Oktoba 13
alitakiwa kuwa mapumziko na alitakiwa kazini Oktoba 14 lakini
hakuonekana.
Inasemekana
juhudi za kumtafuta zilianza kufanyika ambapo simu zake za mkononi
zilipopigwa ziliita bila majibu na ndipo ufuatiliaji ulifanyika hadi
mahali alipokuwa akiishi ambapo alikutwa yeye pamoja na mwenzake wakiwa
wamefariki dunia ndani ya chumba chao cha kulala huku miili yao ikiwa
haina jeraha lolote.
Katika
eneo la tukio kulikutwa madawa mbalimbali ya usingizi aina ya Dayaspem,
dawa za hospitali, Panadol, vichungi vya sigara, sigara aina ya Cornel
yenye unga unga unaodhaniwa ni dawa za kulevya, chupa ya maji aina ya
Kilimanjaro yenye maji ndani yake, chupa ya bia aina ya Castlelite ikiwa
nusu na unga unaodhaniwa kuwa ni dawa za kulevya.
Kwa
mujibu wa taarifa hiyo, vifo hivyo huenda vimesababishwa na unywaji wa
pombe kupita kiasi na matumizi ya dawa za kulevya. Miili ya marehemu
imehifadhiwa Hospitali ya Taifa Muhimbili kwa uchunguzi.