MTUHUMIWA wa matukio ya kigaidi na
umwagiaji watu tindikali katika miji mbalimbali nchini ikiwa pamoja na
Arusha, Yahaya Hassan Hela (31) maarufu kama Yahaya Sensei amezikwa
usiku wa `manane’ kijijini kwao Chemchem, kata ya Suruke wilayani
Kondoa, Dodoma.
Sensei aliuawa na polisi wakati akijaribu kuwatoroka baada ya kupambana nao wakiwa kwenye gari.
Kwa mujibu wa chanzo chetu cha habari,
akiwemo shemeji wa marehemu aliyekataa kutajwa jina gazetini, mwili wa
Sensei ulizikwa juzi saa 6 usiku kwa kile kilichoelezwa wanandugu
walihofia kusumbuliwa na vyombo vya ulinzi na usalama.
Mtoa habari wetu ambaye ni mkazi wa kata
ya Daraja Mbili jijini Arusha, alisema alipigiwa simu na baba mzazi wa
Sensei, Mzee Hassan Hela aliyeamuru mwili wa mtoto wake usafirishwe na
kufikishwa kijijini kwao haraka.
Alisema mwili wa Sensei aliyeuawa baada
ya kupambana na polisi usiku wa kuamkia Jumatatu wakati akisafirishwa
kwenda Kondoa ili aoneshe sehemu ya mabomu aliyoyaficha huko,
ulichukuliwa hospitali juzi saa 5 asubuhi hadi Daraja Mbili tayari kwa
kusafirishwa kuelekea kijijini kwa maziko.
‘’Tulimzika juzi usiku kutokana na mwili
kuharibika na isingekuwa busara kuacha hadi siku inayofuata na watu
waliohudhuria hawakuwa wengi.
“Ukiondoa sababu hiyo, ndugu waliamuru
mwili uzikwe usiku wa saa 6 kwa sababu za kiusalama,” alisema mtoa
habari huyo aliyeongeza kuwa, licha ya kuuhifadhi mwili wa Sensei usiku
mwingi, lakini taratibu zote za kidini zilifuatwa.
Sensei aliyekuwa mwalimu wa kareti na
judo mwenye cheo cha `Mkanda Mweusi’ katika fani hiyo, alikuwa mkazi wa
Mianzini, Arusha aliuawa baada ya kutumia taaluma yake hiyo kupigana na
Polisi wakiwa garini majira ya saa 5 usiku na aliporuka kutoka kwenye
gari aweze kukimbia, polisi walimuwahi kwa risasi na kumsababishia
mauti.
Kwa mujibu wa Kamanda wa Polisi mkoani,
Liberatus Sabas, Sensei alikamatwa baada ya kukiri kuhusika katika
matukio tisa ya ulipuaji wa mabomu na umwagiaji watu tindikali katika
mikoa ya Arusha, Dar es Salaam, Mwanza na Zanzibar.
Shekhe Farid Wakati mtuhumiwa huyo
akizikwa huko Kondoa, jijini Dar es Salaam Mahakama ya Hakimu Mkazi
Kisutu, imeshindwa kutoa uamuzi wa ombi la kufutiwa mashitaka ya ugaidi
yanayomkabili Kiongozi wa Jumuiya ya Uamsho, Shekhe Farid Hadi Ahmed na
wenzake kwa kuwa jalada halisi la kesi hiyo limepelekwa Mahakama Kuu
Kanda ya Dar es Salaam.
Kesi hiyo ilitajwa jana mbele ya Hakimu
Mkazi Hellen Riwa kwa ajili ya kutolewa kwa uamuzi wa ombi hilo
lililokuwa limewasilishwa na washitakiwa ambapo Hakimu Riwa alisema
hawezi kutoa uamuzi wa ombi hilo kwa sababu jalada halisi la kesi hiyo
limeitishwa Mahakama Kuu, akaahirisha kesi hadi Novemba 4 mwaka huu
itakapotajwa tena.
Washtakiwa hao waliwasilisha ombi
wakiiomba Mahakama ifute kesi hiyo kwa sababu hati ya mashitaka iliyopo
mbele ya mahakama hiyo ina mapungufu.
Washitakiwa wengine katika kesi hiyo ni
kiongozi mwingine wa Jumuiya hiyo Shekhe Mselem Mselem ambaye pamoja na
Shekhe Ahmed wanatuhumiwa kuwaajiri watu waliotenda vitendo vya kigaidi.
akiwamo Abdallah Said Ali. Katika
mashita mengine yanayowakabili pamoja washitakiwa wengine 19, inadaiwa
katika tarehe tofauti kati ya Januari, 2013 na Juni, 2014 katika maeneo
mbalimbali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, washitakiwa wote walikula
njama ya kutenda kosa kinyume cha Sheria ya Ugaidi ya mwaka 2002, kwa
kuingiza watu kushiriki vitendo vya kigaidi.
Aidha, washitakiwa wanadaiwa kuwasaidia watu hao kufanya vitendo vya ugaidi.
Na John Mhala, Arusha na Flora Mwakasala