Mgogoro wa kifamilia kuhusu mwenye haki ya kuzika mwili wa
Rosemary Marandu (38), umeingia siku ya 43 leo, huku ukiendelea
kuhifadhiwa Hospitali ya Rufaa ya KCMC.
Mwili wa marehemu huyo aliyefariki dunia Septemba
4, mwaka huu umehifadhiwa hospitalini hapo na unalipiwa Sh9,000 kwa
siku, gharama ambayo hadi leo imefika Sh387,000.
Akizungumza jana, baba wa marehemu, Flavian
Marandu, alitoa ruksa ya kuzikwa mwili huo, huku akijiweka kando akidai
hana mamlaka ya kuzika mke wa mtu.
Wiki moja iliyopita, mume wa marehemu, Sigfrid
Mlingi alimtuhumu baba mkwe wake huyo kuzuia mwili huo na baadaye
kumtolea lugha chafu.
“Mimi ndiye nilimuuguza Hospitali ya Mawenzi hadi
kunifia mikononi, nilipokwenda Keryo na kuonana na baba mkwe,
akanifukuza,” alidai Mlingi.
Mlingi alisema awali walikubaliana kumzika
Septemba 9 katika Makaburi ya Karanga, Manispaa ya Moshi lakini baadaye
mkwewe alikataa.
Lakini jana, Marandu alisema: “Huyo ni mke wa
mtu...kama kuna mtu ana shida akachukue kibali akazike, mimi sina
kibali,” alisema.
Marandu alisema tangu msiba huo utokee, ametuma
marafiki zake kuzungumza na ndugu ili mazishi hayo yafanyike baada ya
kuridhiwa na mume na mama mzazi lakini hawatoi ushirikiano.
Lakini ndugu mwingine wa marehemu, Bertha Akwilin
alipoulizwa jana, alikiri kuzungumza na Marandu juzi na kumwelekeza
kwenda kuchukua kibali kutoka kwa mtu aitwaye Tesha.
“Ni kweli nimepata bahati ya kuzungumza na baba
(Marandu) na akatoa ruksa hiyo lakini mama wa marehemu na wana ndugu
bado wanatafakari ukweli wa kauli ya Marandu,” alisema.
Na Daniel Mjema, Moshi
Na Daniel Mjema, Moshi