CHADEMA KAHAMA WACHAPANA MAKONDE KUPINGA WENZAO KUENGULIWA KWENYE UCHAGUZI

Na Raymond Mihayo
UCHAGUZI wa ndani wa Chama cha Chadema wilayani Kahama mkoani Shinyanga umeingia dosari baada ya baadhi ya wagombea na wanachama kuchapana makonde kupinga kuenguliwa kwa baadhi ya majina ya wagombea katika uchaguzi wa Baraza la Vijana wa chama hicho (BAVICHA).

Ugomvi huo ulitokea baada ya wagombea waliopitishwa katika nafasi ya uenyekiti kuanza kujinadi kwa wanachama, ndipo mgombea mmoja aliyeenguliwa (jina tunalo) kwa maelezo hana sifa alipojitokeza kuzuia uchaguzi.

Kitendo hicho kiliungwa mkono na wafuasi wake wakiwemo wa kikundi cha ulinzi wa chama cha Red Brigade, na kuanzisha fujo.

Hali hiyo ilikwenda mbali zaidi kwani wafuasi hao walianza kuwashambulia baadhi ya viongozi na wasimamizi ambapo Mwenyekiti wa Chadema wa Halmashauri ya Msalala, Emmanuel Bombeda alipigwa ngumi na vijana wa Red Brigade wanaomuunga mkono mgombea aliyeenguliwa.

Hata hivyo, hali ilirejea kuwa shwari baada ya Msimamizi wa Uchaguzi wa chama hicho Kanda ya Ziwa Mashariki, Madata Benard Sande kuingilia kati na kuwataka wanachama kuwa wavumilivu ili kufanikisha uchaguzi huo ikielezwa walioenguliwa hawakuonewa, kwa mujibu wa Katiba ya chama hicho.

Katika uchaguzi huo, Diwani wa Kata ya Naysubi, Leonard Mayala aliyekuwa anawania nafasi ya Mwenyekiti wa Wilaya, naye alienguliwa, kwa sababu za kimaadili.

Baada ya kuzimwa kwa vurugu na uchaguzi kuendelea, Juma Protas alichaguliwa kuwa Mwenyekiti wa Chadema wilayani Kahama, huku nafasi ya Katibu ikienda kwa Mshibu Peter. Kwa upande wa Bavicha, Samwel Peter alichaguliwa kuwa Mwenyekiti.


JIUNGE NA EDMO BLOG SASA

Usipitwe!! Jiunge nasi kupitia Facebook,Twitter na Instagram ili kupata habari zote za town! Usikose kujiunga na Youtube kuangalia video zote kali kutoka Edmo Blog Pekee!, kujiunga bonyeza hapa>>>Youtube

Tupe Maoni Yako lakini Usiandike Matusi



 
© Copyright EDMO BLOG | Designed By Peruzibongo