Mwenyekiti wa chama hicho wilayani humo, Nikolaus Kilunga, amesema
wakazi wengi wa Kibondo mjini na vijijini wanatumia nishati ya mkaa na
kuni hivyo kauli ya serikali kuwazuia ghafla bila kufanya maandalizi ni
kuwapa adha wananchi wanaotegemea nishati hiyo.
“Tunapenda kutoa tamko la kupinga uamuzi wa Halmashauri kuzuia uuzaji
wa mkaa na kuni bila kuwa na maandalizi ya kutosha kwa kutoa taarifa kwa
wahusika, kwani hawajatoa elimu wala kuangalia athari za kiuchumi na
kijamii kwa wakazi wa wilaya nzima ya Kibondo zinazoweza kutokea mara
baada ya kufanya maamuzi kama haya” alikaririwa
Aidha, ameeleza kuwa kwamba wameieleza idara husika kuhakikisha inakaa
pamoja na wauzaji na watumiaji wa mazao hayo, sambamba na kutoa elimu
juu ya namna ya utunzaji wa mazingira pamoja na tozo wanazotakiwa kutoa
ili wananchi waweze kuelewa jambo wanalolifanya.
Katika hatua nyingine, chama hicho kimetoa siku saba (7) kwa serikali
kubatilisha maamuzi yake na kukaa na wadau wote ikiwa ni pamoja na
watumiaji na wauzaji wa mkaa na kuni, ili kutoa elimu ya mali
zinazozunguka wananchi na namna ya kuzitumia, elimu ya kodi na tozo
nyingine ili kuepusha mzozo usio wa lazima kwa wananchi wanaopata kipato
kidogo kutokana na kutegemea mazao hayo.
Wananchi wa Wilaya hiyo wakiongea kwa nyakati tofauti
leo Agosti 25, 2014, wamedai serikali kuendeleza zuio hilo bila
utaratibu maalumu ni ukiukwaji wa haki za binadamu na kuwanyima wananchi
mahitaji ya lazima kwani hawataweza kupika kutokana na kutegemea kuni
na mkaa kwa ajili ya kupikia na kuuza kwa ajili ya kujitafutia kipato
cha familia zao.
Kwa upande wa wafanyabiashara wa mkaa mkoani humo akiwemo Jovita
Nyuntwa, wamesema hatua hiyo imewafanya waishi kwa kuhangaika kutokana
na kupewa muda mfupi wa kuacha kufanya biashara hiyo Agosti 22, 2014
huku wakisema watumiaji wa nishati hiyo wameonekana kupata adha kubwa
kutokana na kusitishwa kwa huduma hiyo.
Meneja Misitu katika Wilaya hiyo, Rojas Simon, amekiri kuwepo kwa suala
hilo na kusema “Mimi suala langu ni kuhakikisha ninasimamia kuwa sheria
inafuatwa na ninapenda nirudie kwamba hatujamzuia mtu kufanya biashara
ya mkaa bali tunamruhusu mtu ambaye amefuata taratibu za sheria za
misitu ili afanye biashara na siwezi kumuacha mtu akavunja sheria
kwasababu eti kuna hali ngumu ya maisha".
Nishati ya mkaa na kuni katika Wilaya ya Kibondo mkoani humo,
imeonekana kuuzwa kwa magendo na kwa bei ya juu kati ya shilingi 44,000
kwa gunia hadi shilingi 50,000 hali ambayo imelalamikiwa na baadhi ya
wauzaji na watumiaji kabla ya zuio hilo.
CHANZO:FikraPevu
