MAJAMBAZI YAFUNGWA JELA MIAKA 270 HUKO CHUNYA MBEYA


Mahakama ya Hakimu Mkazi Wilaya ya Chunya mwishoni mwa wiki iliwahukumu watu tisa kwenda jela jumla kwa miaka 270 baada ya kupatikana na hatia ya wizi wa kutumia silaha. 
 
Washtakiwa hao ni Samweli Sarehe (40), Bahati Kenson (29), Aulesi Andason (28) na Ayubu Swila (24), wote wakazi wa Mbalizi  Wilaya ya Mbeya Vijijini.
 
Wengine ni Mathias Simfukwe (31), Pascal Simchimba (27) wote wakazi wa  Kijiji cha Kanga Wilaya ya Chunya, Tegemea Kenya (27) mkazi wa Kijiji cha Mjele, Shukuru Mwakatumbula (27) wa Ifumbo na Maleba Kindagilo (46) wa Lupa, Chunya.
 
Awali, ilielezwa mahakamani hapo na mwendesha mashtaka wa polisi, Raymond Lukomwa kuwa washtakiwa  wote kwa pamoja walifikishwa mahakamani hapo Desemba 27, 2013 kwa kosa moja la wizi wa kutumia silaha  kinyume na Kifungu cha 287A cha Sheria ya Adhabu, Sura ya 16 iliyofanyiwa marekebisho 2012.
 
Alidai kuwa washtakiwa walifanya kosa hilo Desemba 14, 2013 katika eneo la Kasangakanyika ambako waliiba vipimo vitano vya dhahabu vyenye thamani ya Sh58 milioni na fedha tasilimu Sh6milioni, mali ya Paul Sinjale (44) na kwamba katika wizi huo walitumia bunduki aina ya shortgun.
 
Akisoma hukumu hiyo, Hakimu Mkazi wa Wilaya ya Chunya, Desdeli Magezi alisema kwa mujibu wa Kifungu cha Tano (A) (ii) cha Sheria ya Adhabu, Sura ya 90 iliyofanyiwa marekebisho mwaka 2002 wote kwa pamoja wanahukumiwa kifungo cha miaka 270 na kila mmoja atatumikia kifungo cha miaka 30 jela.


JIUNGE NA EDMO BLOG SASA

Usipitwe!! Jiunge nasi kupitia Facebook,Twitter na Instagram ili kupata habari zote za town! Usikose kujiunga na Youtube kuangalia video zote kali kutoka Edmo Blog Pekee!, kujiunga bonyeza hapa>>>Youtube

Tupe Maoni Yako lakini Usiandike Matusi



 
© Copyright EDMO BLOG | Designed By Peruzibongo