Na Martha Magessa-Iringa
WAKALA wa
Barabara Tanzania (Tanroads) Mkoa wa Iringa imekiri kuzidiwa nguvu na
waharibifu wa miundombinu ya barabara eneo la Ndiuka barabara kuu ya
iringa morogoro, manispaa ya Iringa.
Meneja wa
Tanroads Mkoa wa Iringa, Mhandisi Paulo Lyakurwa ameomba msaada wa
jeshi la Polisi katika kukabiliana na waharibifu hao ambao ni madereva
wa magari makubwa ya mizigo na vijana waosha magari wanaotumia eneo la
maegesho kuosha na kufanya matengenezo ya magari yao.
Amesema
maafisa wa Tanroads wamekuwa wakitishiwa na waharibifu hao kila
wanapojaribu kuwakamata kwa kukiuka sheria za barabara na wanaofanya
matengezo, kuosha au kupata ajali huaribu miundombinu ya barabara na
kukiuka sheria ya Barabara Namba 13 ya mwaka 2007 kifungu cha 54
kinachowataka kulipa faini, kama fidia ya kukarabati au kuirejesha kama
ilivyokuwa.
Hata
hivyo mhandisi Lyakurwa ameongeza kuwa maegesho hayo hayakujengwa kwa
ajili ya matengenezo ya magari yao wala kwa ajili ya kuosha magari yao
watambue kwamba mafuta ya magari, maji na sabuni vikikaa kwa muda mrefu
barabarani vinafifisha ubora wa lami na hatimaye uharibifu.
Kwa
upande wake Mkuu wa Mkoa wa Iringa, Dk Christine Ishengoma alimuomba
Mkuu wa Wilaya ya Iringa, Mkurugenzi wa Halmashauri ya Manispaa ya
Iringa na Mstahiki Meya wa Manispaa ya Irinnga kuwatafutia eneo mbadala
vijana wanaofanya biashara ya kuosha magari katika eneo hilo.
