Mtalii kutoka nchini Ujerumani anayefahamika kama Bi. Jeanne Traska (32) akiwa na muongoza wageni Athuman Juma leo majira ya saa mbili na nusu asubui wamekwama katika kilele cha Mawenzi Mlimani Kilimanjaro kwa kamba iliyonasa na kuwafanya wasiweze kushuka chini wala kwenda juu.
Bi. Jeanne na Athuman Juma walianza kupanda
mlima kupitia Kampuni ya Nordic Tours tarehe 18.3.2014 kwa kutumia njia ya
Rongai - Kibo –Marangu safari ambayo ingewachukua siku tano.
Hadi sasa taarifa
za awali zinaonyesha kuwa Bi. Jeanne alitakiwa kwenda kileleni Kibo lakini
katika mazingira yasiyofahamika alibadili uamuzi na kuelekea kilele cha Mawenzi
ambacho huwa hakitumiwi na watalii isipokuwa kwa kujaza fomu maalum
inayoonyesha kuwa mgeni amekubali kwa hiyari yake kupanda kilele hicho.
Shirika la Hifadhi za Taifa kwa
kushirikiana na Kampuni ya Nordic Tours wanaendelea na jitihada za uokoaji kwa
kutumia askari ambao wanaelekea eneo la tukio pamoja na helikopta itakayosaidia
zoezi la uokoaji kwa kutegemea na hali ya hewa itakavyotulia ambapo hivi sasa
kuna mawingu mazito katika eneo la mlima.
Umma utaendelea kufahamishwa maendeleo
ya jitihada za uokoaji kadri zitakavyopatikana.
Imetolewa na
Idara ya Mawasiliano
Hifadhi za Taifa
Tanzania
22.03.2014
