NYUMBA ya Baba wa Taifa, Mwalimu Julius
Nyerere, inayotumiwa na mjane wake, Mama Maria na familia, wiki hii
imevamiwa na vibaka usiku na kuvunjwa. Taarifa zilizofikia gazeti hili
jana zilibainisha kuwa vibaka hao walipitia upande wa ufukweni usiku wa
manane, wakavunja dirisha na kuingia.
Kwa mujibu wa taarifa hizo, vibaka hao
walitoweka na televisheni, ambayo haikutajwa aina wala ukubwa na
kompyuta ya mkononi aina ya Toshiba.
Akizungumza na gazeti hili, Kamanda wa
Polisi wa Mkoa wa Kinondoni, Camilius Wambura, alisema nyumba hiyo
ilivamiwa Januari 11 kati ya saa 8 usiku na alfajiri.
Alithibitisha kuwa wezi hao waliingia
ndani ya uzio na kuiba televisheni na kompyuta mpakato. Kamanda Wambura
alisema kabla ya saa 8 usiku kuna watu walikuwa macho, lakini baada ya
muda walikwenda kulala na walipoamka asubuhi wakakuta wameibiwa.
"Ndani ya uzio huo kwa pembeni kuna
nyumba anamoishi mjukuu wa Mwalimu Nyerere, na huko ndiko waliingia na
kuiba televisheni na hiyo kompyuta baada ya kukata waya wa dirisha,"
alisema Kamanda Wambura.
Alisema taarifa ya tukio hilo imefunguliwa jalada katika kituo cha Polisi Oysterbay na kupewa namba OB/RB/822/2014.
Kamanda alimtaja mjukuu wa Mwalimu
aliyeibiwa kuwa ni Moringe Nyerere (30), ambaye anafanyakazi katika
Shirika la Taifa la Hifadhi ya Jamii (NSSF), na anaishi katika nyumba
hiyo.
Kwa mujibu wa Kamanda Wambura, tayari
mtu mmoja amekamatwa akihisiwa kushiriki wizi huo ambaye hakumtaja jina,
lakini alisema alipata kufanya kazi katika nyumba hiyo na baadaye
kufukuzwa.
"Kuna kijana walimhisi kufanya wizi huo
ambaye alikuwa akifanya kazi hapo kwa karibu miaka miwili lakini
alifukuzwa kutokana na tabia ya udokozi, siku mbili kabla ya wizi huo
alionekana hapo na alipoondoka wizi huo ukafanyika," alisema Kamanda
Wambura na kuongeza kuwa kuna mtuhumiwa mwingine anatafutwa.
CHANZO:http://habarileo.co.tz
