Wakala wa madini nchini TMAA imesema serikali imepata hasara ya zaidi ya shilingi milioni 547.15 zilizosababishwa na utoroshaji
wa madini kwenda nje ya nchi kupitia viwanja vya ndege vya Dar Es
Salaam, Kilimanjaro na Mwanza katika kipindi cha miezi mitatu kuanzia
Oktoba hadi Desemba mwaka 2013.
Kadhalika serikali imeendelea kupata hasara ya shilingi bilioni 2
kutokana na kesi 32 kupelekwa mahakamani kwa mwaka 2013 pekee.
Kutokana na ukaguzi uliofanywa na Taasisi mbalimbali za Serikali
imebainika kuwa maeneo ya mipakani na sekta ya usafirishaji ndiko kwenye
uhalifu mkubwa wa utoroshaji wa madini hatua inayoifanya Wakala wa
Madini Tanzania TMAA kuiomba Serikali kuzidisha nguvu zaidi katika
maeneo hayo.
Ingawa TMAA imekuwa ikifanya jitihada za kudhibiti utoroshaji wa madini
hayo, imebainika kuwa wanaofanya uhalifu huo ni Watanzania na Raia wa
Kigeni na kwamba changamoto kubwa ni kutoroka kwa wahalifu hao wakiwa
katika vyombo vya usalama.
Kufuatia hali hiyo Wakala hao wakatoa onyo dhidi ya wanaofanya uhalifu
wa utoroshaji madini hayo na kuwataka Watanzania kutosita kutoa taarifa
kwa vyombo husika.
Tangu kuundwa kwa Wakala wa Madini Tanzania Mwaka 2012 kesi 37
zimeripotiwa Mahakamani zilizotokana na uhalifu huo ambazo kwa asilimia
kubwa zimekuwa zikitokea kwenye viwanja vya Ndege
