Serikali imependekeza ongezeko la adhabu kwa magazeti yanayochapisha
habari zinazoweza kusababisha uchochezi au uvunjifu wa amani katika
jamii kutoka faini ya shilingi elfu 10 na 5 hadi kiasi kisichopungua
shilingi milioni 5.
Akiwasilisha mswada wa sheria ya marekebisho ya
sheria mbalimbali wa mwaka 2013, mwanasheria mkuu wa serikali jaji
mstaafu Fredrick Werema, amesema marekebisho hayo yanalenga kutekeleza
azimio la bunge lililotolewa katika mkutano wa 11 kikao cha 21 ambalo
bunge liliazimia serikali kupitia sheria zilizopo ili kuona kama
zinatosheleza kuzuia lugha ama kauli za uchochezi.
Wakiwasilisha maoni ya kamati ya katiba, sheria na
utawala, pamoja na maoni ya kambi ya upinzani, msemaji wa kamati hiyo
Mhe Fakharia Shomar amesema kamati yake inaunga mkono pendekezo la
serikali kwa kuzingatia misingi ya vyombo vya habari ni kuelimisha na
kuhabarisha si kuleta uchochezi,wakati kambi rasmi ya upinzani bungeni
imeitaka serikali kufuta sheria na kutunga sheria mpya itakayojali uhuru
wa vyombo vya habari.
Wakichangia mswada wa sheria ya marekebisho ya
sheria mbalimbali baadhi ya wabunge wameitaka serikali kuharakisha
kuleta mswada wa sheria vyombo vya habari,huku wengine wakipinga adhabu
ya shilingi milioni 5 kwa madai kuwa ni kiwango kikubwa na kutaka
serikali kuweka uwiano kwa baadhi ya watu wanaopinga kutoa taarifa kwa
vyombo vya habari.
Via ITV Habari 20:00hrs
