KURA ZAENDELEA KUHESABIWA NCHINI ZIMBABWE

Epworth, Zimbabwe
Wapiga kura wakiwa kwenye foleni mjini Epworth, Zimbabwe Julai 31, 2013. Picha/Habari na AFP
  
HARARE, Zimbabwe.
Kura zinaendelea kuhesabiwa nchini Zimbabwe, baada ya uchaguzi mkuu wenye ushindani mkubwa uliofanyika mnamo Jumatano. Wapiga kura wengi walijitokeza kushiriki, huku kukiwa na madai ya njama za wizi wa kura na wandani wakuu wa rais Robert Mugabe, ili kuendeleza utawala wake wa miaka 33.

Mpinzani wake mkuu, Bw Morgan Tsvangirai, alinukuliwa akisema kuwa anatarajia uchaguzi huo kuwa mwanzo mpya kwa taifa hilo la kusini mwa Afrika.

Waandalizi waliripoti kuwa idadi kubwa ya wapiga kura ilijitokeza katika uchaguzi huo, ulio wa kwanza nchini humo tangu uchaguzi mkuu wa 2008 uliogubikwa na ghasia, na uliopelekea kubuniwa kwa serikali ya muungano kati ya viongozi hao wawili.

Hakukuwa na ripoti zozote za uwepo wa ghasia, licha ya kampeni kali zilizojawa na utoaji wa propaganda kati ya wapinzani wakuu.

Katika vituo vingi, wapiga kura walianza kupiga foleni kabla ya jua kuchomoza, saa kadha kabla ya kufunguliwa rasmi kwa vituo hivyo.

Upigaji kura uliendelea vizuri, hadi saa za jioni, huku wengine wakilazimika kupiga kura kwa mwangaza wa mishumaa.

Waandalizi walisema kuwa wapiga kura waliokuwa wakingojea katika foleni sharti wangepata nafasi ya kupiga kura zao.

“Watu wote walio katika foleni wanapaswa kuruhusiwa kupiga kura zao, hata ikiwa watafanya hivyo saa sita za usiku,” akasema Bi Rita Makarau, mwenyekiti wa Tume ya Uchaguzi ya nchi hiyo.

Rais Mugabe alipiga kura saa za asubuhi, katika kitongoji kimoja mjini Harare, alikosema kuwa uchaguzi huo utaendana na matakwa ya wananchi.

“Ninaamini kuwa watu watapiga kura kwa amani na hakuna anayeshurutishwa kufanya uamuzi asioutaka,” akasema rais huyo.

Rais Mugabe alipata umaarufu baada ya kuiongoza nchi hiyo katika harakati za kupigania uhuru kutoka kwa Waingereza.

Haki
Lakini utawala wake unaoungwa mkono na jeshi umekuwa ukikumbwa na migogoro ya kiuchumi pamoja na kuhujumiwa kwa haki za kibinadamu, hali ambayo imepelekea nchio hiyo kutengwa na jamii ya kimataifa pamoja na kuwekewa vikwazo na mataifa ya Magharibi.

Mnamo Jumanne, Bw Mugabe aliapa kung’atuka mamlakani, ikiwa Bw Tsvangirai angeibuka mshindi.

“Ukishindwa sharti ukubali,” akasema.”Hatujahusika na njama zozote za udanganyifu,” akaongeza rais huyo.
Lakini Bw Tsvangirai, aliye waziri mkuu, alisema kuwa hakikisho hilo litaaminika likitekelezwa.

Bw Tsvangirai alishinda katika duru ya kwanza ya uchaguzi mnamo 2008, lakini akadinda kushiriki katika duru ya pili ya uchaguzi huo, baada ya waungaji wake mkono 200 kuuawa huku maelfu wakijeruhiwa katika mashambulizi yaliyoonekana kuungwa mkno na serikali.

Bw Tsvangirai mwenye umri wa miaka 61, amekuwa akishikilia  kuwa kuna njama ya kuiba kura katika uchaguzi huo.


JIUNGE NA EDMO BLOG SASA

Usipitwe!! Jiunge nasi kupitia Facebook,Twitter na Instagram ili kupata habari zote za town! Usikose kujiunga na Youtube kuangalia video zote kali kutoka Edmo Blog Pekee!, kujiunga bonyeza hapa>>>Youtube

Tupe Maoni Yako lakini Usiandike Matusi



 
© Copyright EDMO BLOG | Designed By Peruzibongo